SUAMEDIA

Watanzania watakiwa kuchangamkia fursa ya biashara ya Kaboni

 

Na: Farida Mkongwe

Wananchi, makampuni na watu binafsi wametakiwa kujitokeza kwa wingi kuchangamkia fursa ya biashara ya Kaboni ambayo inalenga kupunguza gesi joto na kuwajengea wananchi maendeleo endelevu wakiwemo wakulima na wafanyabiashara.

                            

Wito huo umetolewa Agosti 3, 2024 na Mhadhiri Mwandamizi na Msaidizi wa Mratibu wa Kituo cha Kitaifa cha Ufuatiliaji wa Kaboni nchini kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) Dkt. Deo Shirima wakati akizungumza na SUA Media katika banda la Chuo hicho  kwenye Maonesho ya Nane nane Kanda ya Mashariki yanayoendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere mjini Morogoro.

“Kama alivyosema Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na kauli mbiu ya nishati safi ya kupikia, biashara ya kaboni inatoa fursa kama motisha kwamba tunapofikia lengo la nishati safi kwa maana tunabadilishana nishati ile iliyokuwa inachafua mazingira kwenda kwenye nishati safi ya kupikia lakini wakati huo huo tunapata faida ya ziada au motisha kwa kupitia biashara ya kaboni”, amesema Dkt. Shirima

                                

Dkt. Shirima ametoa wito kwa makampuni ambayo yanajikita kwenye kauli mbiu hiyo ya Serikali ya nishati safi ya kupikia yafikirie kuongeza eneo la biashara ya kaboni katika miradi yao na pia kwenye masuala ya mazingira, kilimo na biashara ambayo inaweza kuwa fursa nzuri ya kusaidia kuongeza motisha kwa kutunza mazingira na kufaidika na biashara ya kaboni kama utasajili kuwa sehemu ya biashara hiyo.

“Mpaka sasa Kituo kimesha sajili miradi ya kaboni zaidi ya 50 na miradi hiyo ipo katika sekta mbalimbali, miradi mitatu tayari imeshaanza kufanya kazi na kutoa faida na wananchi wameshaanza kunufaika, unaweza kufanya miradi hii katika sekta mbalimbali mojawapo ambayo watu wanaweza kuwekeza ni kwenye sekta ya misitu ambayo mpaka sasa tuna hekta takribani milioni 19 ambazo wameshajitokeza wawekezaji wanataka kuwekeza”, amesema Dkt. Shirima.

                            

Amesema miradi hiyo inaweza kusajiliwa kwa kuzingatia kanuni inayosimamia uwekezaji wa miradi ya kaboni nchini na kwamba watu wanaweza kujiunga kama kikundi wakajisali kwenye biashara ya kaboni na kitu kikubwa zaidi na kizuri ambacho kimewekwa kwenye kanuni ni kwamba ni lazima kuona namna gani wale wanaozunguka rasilimali za hapa nchini mfano misitu, nishati, kilimo wanafaidika na biashara yenyewe..

“Chimbuko la biashara hii ni kama tunavyofahamu kumekuwa na ongezeko la gesi joto duniani na hivyo mataifa ulimwenguni kote yakataka kuhakikisha tunapunguza ongezeko hilo, sasa ili kufikia azma hiyo ndiyo kukawa na utaratibu wa kuzitaka nchi ambazo zimeendelea na kuzalisha gesi joto kwa wingi zione namna gani ya kuweza kuingia kwenye mfumo wa kimasoko ambao utafanya wale watakaokupunguza gesi joto waweze kupata motisha na hivyo kutengeza fursa ya kibiashara”, amesema Mhadhiri huyo.

 
PICHA NA TATYANA CELESTINE









Post a Comment

0 Comments