SUAMEDIA

Wafugaji wa kuku wametakiwa kutumia teknolojia mpya ya uhimilishaji ili kupata mazao bora

 Na: Farida Mkongwe

Wafugaji nchini wametakiwa kutumia teknolojia mpya ya uhimilishaji wa kuku inayopatikana katika Chuo  Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) ambayo inatoa nafasi kwa mfugaji kuchagua aina ya mbegu bora ya kuku anaotaka kufuga ambao watakuwa na uzalishaji utakao mletea faida.

                                    

Teknolojia hiyo imewekwa bayana na Afisa Mifugo Mwandamizi Bi. Enesa Mlay kutoka Ndaki ya Tiba ya Wanyama na Sayansi za Afya SUA wakati akizungumzia namna ya kupata mbegu bora za kuku wa asili katika Maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki yanayoendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere mjini Morogoro.

Akizungumzia namna teknolojia hiyo inavyofanya kazi Bi. Enesa amesema kinachofanyika katika uhimilishaji ni kuwa kunakuwa na majogoo na majike ambapo inatolewa mbegu kwa majogoo na kuiweka kwenye njia ya uzalishaji wa majike hali inamuwezesha mfugaji kupata vifaranga kutokana na mbegu aliyoichagua.

                                      

“Sasa hivi wafugaji wetu tunawaelimisha kuwa wasikae na majogoo na matetea ambao ni ndugu au ni wa ukoo mmoja kwa sababu wakipandana wakati ni ndugu wakati mwingine jogoo anampanda tetea ambaye ni mtoto wake au dada yake hii inaleta changamoto  katika kupata kuku wenye ubora hivyo njia hii ya uhimilishaji ni teknolojia sahihi ya kuondoa changamoto hii”, amesema Afisa Mifugo huyo.

Amezitaja changamoto za kuku kupandana wakiwa ndugu au ukoo mmoja kuwa ni kushindwa kupata mbegu bora kwa sababu kuku watakaototolewa watakuwa wadogo kwa umbo, kupata kuku walemavu na dhaifu kiafya pamoja na kukosa muendelezo wa mbegu bora kwa siku zijazo na hivyo kupoteza wazazi bora katika ufugaji wako.








PICHA NA TATYANA CELESTINE



Post a Comment

0 Comments