SUAMEDIA

Kliniki ya Mimea SUA kuwasaidia wakulima nchini kutambua ubora wa mbegu

 

Na: Winfrida Nicolaus

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA kupitia Ndaki ya Kilimo, Idara ya Mimea, Vipando na Mazao ya Bustani imekuja na Kliniki ya Mimea kwa ajili ya kuwasaidia wakulima kote nchini kuweza kutambua ubora wa mbegu na aina ya ugonjwa katika mazao yao na namna ya kudhibiti magonjwa hayo kwa kutumia vifaa vyenye ubora na vya kisasa toka kwenye Kliniki hiyo.

                        

Amebainisha hayo Bw. Isack Kazosi Afisa Kilimo kutoka Idara ya Mimea, Vipando na Mazao ya Bustani, Kitengo cha Kliniki ya Mimea SUA wakati akizungumza na SUAMEDIA katika Maonesho ya Wakulima, Wafugaji na Wavuvi Kanda ya Mashariki kwenye Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere mjini Morogoro.

Amesema wakulima walio wengi wamekuwa wakikutana na changamoto mbalimbali ikiwemo magonjwa katika uzalishaji na ukuzaji wa mazao shambani na wanakosa namna nzuri ya kudhibiti changamoto hizo hivyo kuna umuhimu mkubwa wa kutembelea Banda la SUA kwenye maonesho hayo ili kuweza kukutana na wataalam katika Kliniki hiyo kwa elimu na ushauri juu ya jinsi ya  kutambua tatizo kwenye mmea na namna ya kulidhibiti tatizo hilo.

                                    

“Tunazo mbinu za kutambua ubora wa mbegu hivyo mkulima anaweza kuja na mbegu zake alizo nazo ili kuweza kujua ubora wa mbegu hizo lakini pia endapo kutaonekana na vimelea vitakavyoleta changamoto kwenye uzalishaji na kushindwa kupata mazao stahiki atapata ushauri wa kumuwezesha kupata mazao yenye tija”, amesema Bw. Kazosi.

Aidha Bw. Kazosi amesema kwa yule mkulima ambaye ana mazao tayari shambani na yameshambuliwa na magonjwa na kushindwa kujua namna sahihi ya kudhibiti magonjwa hayo apeleke sampuli kutoka shambani ili iangaliwe na kuweza kutambua aina ya ugonjwa unaosumbua mazao yake na kupatiwa ushauri wa namna sahihi ya kudhibiti .

Maonesho ya Nanenane mwaka huu yamebeba kauli mbiu isemayo “Chagua Viongozi Bora wa Serikali za Mitaa kwa Maendeleo Endelevu ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi”









Post a Comment

0 Comments