SUAMEDIA

Wakulima wametakiwa kufika banda la SUA ili kupata elimu ya teknolojia bora za kilimo

 

Na: Farida Mkongwe

Katika kuhakikisha wakulima, wafugaji na wavuvi wanafaidika ipasavyo na Maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki kwa mwaka 2024, Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimekuja na teknolojia mpya, tafiti na ushauri wa kitaalamu ambao utawasaidia wakulima na wafugaji  kuongeza  uzalishaji wao.

                                        

Hayo yamebainishwa Agosti, 5, 2024 na Mkurugenzi wa Taasisi ya Elimu ya Kujiendeleza (ICE) iliyopo SUA Dkt. Devota Mosha wakati akizungumza na SUA Media kuhusu huduma mbalimbali  zinazotolewa na SUA katika banda lao la  Maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki lililopo katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere mjini Morogoro.

                                         

Dkt. Devota amesema ICE kazi yao  ni kuratibu shughuli zote za maonesho ya Nanenane na kwa mwaka huu wamehakikisha mada zote muhimu zinazohusu wakulima na wafugaji zinapatikana ili kukidhi matakwa ya wakulima ikiwa ni pamoja na mada zinazohusu uzalishaji bora wa wanyama na mifugo ya aina mbalimbali ikiwemo nguruwe, kuku na samaki.

“Kwa ujumla wadau wetu wamefurahi sana kwa namna ambavyo tumejipanga katika maonesho haya na kikubwa kilichowafurahisha ni kuona huduma zote muhimu za kilimo na ufugaji zinapatikana mahali hapa kwa maana kama mtu amekuja kujifunza basi inakuwa ni rahisi kupata huduma nyingi katika eneo moja”, amesema Dkt. Devota.

Mkurugenzi huyo wa ICE ametoa wito kwa wananchi wote wakiwemo wakulima na wafugaji kuhakikisha wanafika katika banda hilo la SUA na wanapofika wasiwe na haraka ya kuondoka ili kupata kujifunza na kufaidika na matunda ya tafiti zilizofanywa na watafiti bora na wabobezi kutoka SUA.

“Wito wangu mkubwa kwa watu wanaokuja kwenye banda letu, banda la SUA lina idara nyingi naomba wanaofika watumie muda mwingi ili waweze kujifunza na kuelewa, hawatakiwi kuwa na haraka kwa sababu kila banda linatoa elimu nzuri yenye manufaa, kwa ujumla mabanda yetu yana lengo la kuboresha kilimo na kwa wafanyabiashara waweze kuwa na biashara zitakazowaongezea kipato na hivyo kukuza uchumi wao na wa Taifa kwa ujumla”, amesema Dkt. Devota






Post a Comment

0 Comments