SUAMEDIA

Wakazi wa Mkoa wa Morogoro watakiwa kufika SUA kupata elimu na ushauri wa kitaalamu juu ya ulaji sahihi

Na: Winfrida Nicolaus

Wakazi wa Mkoa wa Morogoro na maeneo ya jirani wametakiwa kufika kwenye banda la Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) katika Maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki ili kupata elimu na ushauri wa kitaalamu juu ya ulaji sahihi ambao utawaweka mbali na magonjwa.

                            

Amebainisha hayo Dkt. Zahra Majiri Mhadhiri kutoka SUA, Idara ya Sayansi ya Lishe na Stadi za Mlaji wakati akizungumza na SUA Media katika banda la Chuo hicho  kwenye Maonesho hayo yanayoendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere mjini Morogoro.

Amesema Lishe bora ina faida nyingi mwilini kwa kuwa inakufanya uweze kuwa na uwezo wa kuwa na afya bora, uwezo wa kufikiri vizuri na kufanya kazi kwa ufasaha hata kupelekea uwezo wa uzalishaji wenye tija.

                                

“Unapokosa Lishe bora ina maana utakosa nguvu, uwezo wa kufikiri na hata uzalishaji wako utakuwa mdogo, vile vile inaweza kukufikisha kwenye magonjwa mbalimbali hasa yale sugu yasiyoambukiza ikiwemo magonjwa ya moyo, presha na kisukari”, amesema Dkt. Zahra.

Aidha Dkt. Zahra amesema bidhaa yao kuu kwenye maonesho hayo ni kutoa elimu ikiwemo makundi ya vyakula  vile vile kiasi ambacho mtu anahitajika kukipata au kula kwa siku ili afya yake iwe salama lakini pia wanahimiza ufanyaji wa mazoezi kwa ajili ya utunzaji wa afya ya mlaji na kuimarisha mwili.

Ameongeza kuwa licha ya kutoa elimu wanazo pia bidhaa za lishe ikiwemo unga wa uji uliotengenezwa kwa kuzingatia mahitaji ya muhusika lakini pia makundi ya chakula vile vile kuna bidhaa ya biskuti ambayo ipo tofauti na ile ya mtaani inayotumia ngano pekeeambapo wameitengeneza biskuti hiyo kwa kuiongezea thamani kwa kutumia viazi lishe pamoja na mbaazi.

“Sasa hivi tunahamasisha lishe bora kwa watoto kwa kuwa watoto walio wengi imeonekana wana upungufu wa madini ya chuma mwilini vile vile upungufu wa Vitamini A hivyo tumeiongezea thamani biskuti hiyo kwa kuweka viazi lishe na mbaazi ambapo itawasaidia kukutana na madini ya chuma, vitamini mbalimbali na zinki kwa wingi zaidi watakapotumia biskuti hizo”, amesema Dkt. Zahra.

                                 







Post a Comment

0 Comments