SUAMEDIA

Wafugaji wametakiwa kutibu wanyama wao mapema kabla magonjwa hayajawa sugu

 

Na: Farida Mkongwe

Wananchi wanaofuga wanyama wafugwao kama paka, mbwa, mbuzi, ng’ombe na wanyama wengine wakiwemo wanyamapori wametakiwa kufika au kuwasiliana na wataalamu wa Hospitali ya Rufaa ya Wanyama ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) pindi wanyama wao wanapopata changamoto ya magonjwa ili waweze kupata tiba iliyo sahihi.


                                    


Wito huo umetolewa na Profesa Mshiriki Claudius Luziga ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Uzalishaji, Maonesho na Ushauri katika Ndaki ya Tiba ya Wanyama na Sayansi za Afya SUA wakati akizungumza na SUA Media kuhusu huduma zinazotolewa na Hospitali ya Taifa ya Rufaa ya Wanyama iliyopo SUA katika banda la Chuo hicho kwenye Maonesho ya Nane nane Kanda ya Mashariki yanayoendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere mjini Morogoro.

Prof. Luziga amesema hospitali hiyo ina uwezo wa kutibu magonjwa mbalimbali yanayoshambulia wanyama wanaofugwa na kwamba inatibu magonjwa yanayosababishwa na bakteria au virusi, magonjwa yanayoshambulia mifumo ya hewa, kuvunjika na magonjwa mengine yanayowapata  wanyama kwa kutumia vifaa vyenye ubora wa hali ya juu.

                                      

Amesema mbali na magonjwa yanayoshindikana katika kliniki ndogOndogo na kupelekwa kwenye hospitali hiyo ya Rufaa, pia wanaangalia changamoto zinazowakabili wanyama zinazotokana na uzazi .

“Wanyama wanaofugwa ili waweze kuwa na faida ni lazima wazaliane ndipo walete faida na ndiyo maana hata kama kuna changamoto ya mnyama kushika mimba tunaweza kutatua kwa kuwapa dawa au kufanya uhamilishaji kwa sababu SUA tuna mbegu zilizo bora”, amesema Prof. Luziga.

Aidha Prof. Luziga ametoa wito kwa wananchi wanaotembelea Maonesho ya Nane nane Kanda ya Mashariki kufika kwenye banda la SUA ili waweze kupata elimu mbalimbali pamoja na kupata ushauri nasaha kwa mtu anayetaka kuanzisha shamba la wanyama ambapo mtu huyo atapata elimu ya namna bora ya kufuga na kuendeleza mifugo yake.







Post a Comment

0 Comments