SUAMEDIA

Wafugaji wa samaki nchini wametakiwa kutumia teknolojia mpya ya BIOFLOC ili kuzalisha kwa tija

 Na: Farida Mkongwe

Wafugaji wa samaki wametakiwa kutumia teknolojia mpya ya BIOFLOC ambayo ni muunganiko wa mimea midogo midogo na bakteria ambayo huboresha ukuaji wa samaki na kudumisha ubora wa maji kwenye bwawa la samaki na hivyo kumfanya mkulima kufuga kwa tija.

                                

Wito huo umetolewa na Mhadhiri Msaidizi kutoka Idara ya Sayansi ya Wanyama, Ukuzaji Viumbe Maji na Nyanda za Malisho Mariamu Bakari wakati akizungumza na SUA Media kwenye Maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki kuhusu changamoto mbalimbali zinazowakabili wafugaji wa samaki.

                                

Amesema SUA wamekuja na hiyo teknolojia iliyo bora baada ya watafiti wengi kujaribu kuangalia njia mbadala ambayo itaweza kupunguza gharama za chakula na kudhibiti ubora wa maji ambayo yanafugiwa samaki lakini changamoto hiyo bado imeendelea kuwepo.

                               

“SUA tumekuja na teknolojia nyingine ambayo ni bora zaidi inaitwa BIOFLOC, teknolojia hii inafanya kazi kwa kuongeza wanga kwenye bwawa la samaki ambao huongeza uzalishaji wa bakteria ambao huondoa ammonia kwenye bwawa  ambapo chembe chembe za floc ambazo hupatikana baada ya bakteria kuchanganyika na mimea hutumika kama chakula cha samaki”, amesema Mhadhiri huyo.

                                

Amezitaja faida za teknolojia hiyo kwenye ufugaji wa samaki kuwa ni kufuga samaki wengi kwenye eneo dogo yaani zaidi ya samaki 250 kwa ujazo wa mita moja, huongeza kiwango cha kuishi, huongeza ukuaji wa samaki na hupunguza kiwango cha chakula cha samaki.

Faida nyingine ni kuzuia magonjwa ya samaki, huondoa kiasi cha ammonia kwenye bwawa la samaki kwani ammonia ni moja ya vitu ambacho vinaathiri ukuaji wa samaki pamoja na kusaidia katika suala la utunzaji wa mazingira na pia wale bakteria huwa wanakutana na vijimea vidogo vidogo vya asili ambavyo samaki wanakula na hivyo kusaidia kupunguza gharama za chakula.

                                  

“Wafugaji wengi wanakabiliwa na changamoto ya kuhifadhi ubora wa maji, kukosa eneo la kufugia samaki, gharama za chakula ni kubwa na upatikanaji wa maji ya kufugia samaki, hivyo kwa hiyo teknolojia hii itawasaidia kwa sababu mfugaji habadilishi maji kwa miezi yote kuanzia vifaranga hadi mavuno kama ni miezi 5 au 6 na hivyo unatunza mazingira pia”, amesema Mhadhiri huyo.












Post a Comment

0 Comments