SUAMEDIA

 

Na: Winfrida Nicolaus

Wananchi wa Mkoa wa Morogoro na mikoa ya jirani wakiwemo wahitimu wa kidato cha nne na sita wanakaribishwa kutembelea Banda la Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) lililopo   katika viwanja vya Maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki ili kupata elimu juu ya vigezo vya kujiunga na programu za Shahada mbalimbali chuoni hapo, jinsi ya kujisajili pamoja na kupata usaidizi wa moja kwa moja wa kujiunga na Chuo hicho.

                                    

Amebainisha hayo Afisa Udahili wa Shahada za Awali SUA Bi. Grace Kihombo Agosti 3, 2024 wakati akizungumza na SUAMEDIA kwenye Maonesho hayo ambapo amesema dirisha la udahili lipo wazi tangu  Julai 15, 2024 na  litafungwa Agosti 10, 2024 hivyo amewataka wadau wote wenye sifa za kujiunga na Chuo chao  kuwatembelea ili kupata elimu na usaidizi wa kujiunga na Chuo hicho.

“Wakija hapa watapata Elimu kuhusu Shahada tunazozitoa na vigezo vyake, tuna Shahada mbalimbali ambazo SUA tunazitoa  ndani ya Kurugenzi ya Shahada za Awali , tunazo Shahada za Kilimo, Misitu, Ufugaji wa Nyuki vile vile ufugaji wa wanyama  hivyo wakija hapa watapata kuelewa sifa za kujiunga na Shahada hizo”, amesema Bi. Grace.

                                

Aidha Afisa Udahili huyo amesema imekuwa ikieleweka SUA ni kwa ajili ya masomo ya sayansi pekee  lakini pia wanatoa Shahada za sanaa hivyo ametoa rai kwa wananchi na wadau wote ambao wamesoma masomo hayo kujiunga na SUA ili kupata elimu bora, vile vile kwa wale ambao wamemaliza kidato cha nne wanaweza kusoma Astashahada mbalimbali zilizopo chuoni hapo.

Kwa upande wake Bi. Stellah Jacob Afisa Udahili katika Kurugenzi ya Uzamili, Utafiti, Uhaulishaji wa Teknolojia na Ushauri wa Kitaalam SUA amesema wanatoa ushauri wa kitaalama kuhusiana na kozi wanazozitoa kwenye Kurugenzi yao na ushauri kwenye masuala ya Tafiti na Teknolojia mbalimbali zinazozalishwa chuoni hapo.

Ameongeza kuwa dirisha la udahili limefunguliwa tangu Juni 6, 2024 kwa upande wa watu wa shahada za Uzamili (MASTERS) na zoezi hilo litakamilika mwishoni mwa mwezi Oktoba vile vile kwa upande wa watu wa Uzamivu (PHD) hasa zile za course work zitakamilika mwezi Novemba hivyo ni muhimu kufanya udahili kwa kuzingatia muda uliotolewa.

Maonesho hayo ya Wakulima, Wafugaji na Wavuvi kwa mwaka huu 2024 yamebeba kauli mbiu isemayo “Chagua Viongozi Bora wa Serikali za Mitaa kwa Maendeleo Endelevu ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi”.















 

Post a Comment

0 Comments