SUAMEDIA

SUA yaendelea kutoa elimu kwa wanafunzi na wakufunzi kuhusu Elimu ya Mkondo wa Amali

 

Na: Farida Mkongwe

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeendela kutoa elimu kwa wanafunzi wa Chuo hicho lakini pia kwa wakufunzi wa vyuo vidogo, vya kati na vyuo vikuu huku ikiwekea mkazo elimu ya vitendo ili kuwawezesha wahitimu kuwa na ujuzi utakaowawezesha kujiajiri.

                                

Hayo yamebainishwa na Dkt. Hamidu Hassan Khalfan, Mratibu Mkuu wa Shughuli shirikishi za Huduma ambazo SUA kupitia Shule Kuu ya Elimu inazitoa kwa jamii na taasisi mbalimbali zinazoizunguka SUA wakati akizungumza na SUA Media kwenye Maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki mjini Morogoro.

Dkt. Hamidu amesema Wakufunzi wa vyuo lakini pia walimu wa shule za msingi na sekondari wanatakiwa kufundisha kwa mujibu wa mtaala mpya ambao unawataka kufundisha Elimu ya Amali ambayo inahusiana na mazoezi ya vitendo na ujuzi wa moja kwa moja.

                            

“Hii tafsiri yake ni kwamba inaendana na Serikali kwa sasa na badiliko la mitaala ambapo Serikali inatilia mkazo Elimu ya Amali inayojikita katika maendeleo ya uwezo wa kiufundi na kitaaluma kupitia mazoezi na matumizi ya vifaa au mbinu maalum ambayo inapelekea wanafunzi wanaomaliza kidato cha nne au sita au darasa la saba kila mmoja awe na uwezo wa kujiajiri”, amesema Dkt. Hamidu

Amesema katika maonesho hayo ya Nanenane kitu kikubwa wanachokielezea kwenye banda lao ni jinsi walimu watakavyowatengeneza wanafunzi ili wawe wabunifu kwa mujibu wa Elimu ya Mkondo wa Amali ambayo wameipata hivyo walimu wanapoenda kufundisha maana yake waende na nyenzo za kufundishia kwa vitendo.



“Pia inawezekana kabisa anayefundisha au kufundishwa yupo mbali hivyo tumeandaa Application ambayo inaitwa Bright Academy E learning system Architecture, hii inapatikana kwenye play store ya simu yako, kwa kutumia APP hii mtu anaweza kupata elimu ya kitu chochote anachokitaka au maelezo mfano kuhusu mifugo, ujenzi na mengine mengi akaelekezwa na kile chuo alichotoka au mwalimu aliyekuwa akimfundisha akiwa yupo field kwa njia ya mtandao”, amesema Dkt. Hamidu

 


 

Post a Comment

0 Comments