SUAMEDIA

Wakulima washauriwa kutumia teknolojia ya kisasa ya Bundi kudhibiti panya mashambani

 

Na: Farida Mkongwe

Wakulima wameshauriwa kutumia teknolojia ya kisasa ya kuwadhibiti panya waharibifu mashambani kwa kutumia njia ya kibaolojia ambayo inahusisha matumizi ya Bundi katika kudhibiti panya hao ambao wanaharibu mazao.

                                  

Ushauri huo umetolewa Agosti 4, na Mtafiti Msaidizi Teclamageni Mayeji kutoka Taasisi ya Kudhibiti Viumbe Hai Waharibifu katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) wakati akizungumza na SUA Media kwenye Maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki kuhusu teknolojia ya matumizi ya Bundi inavyowasaidia wakulima kuwakomboa na panya waharibifu wa mashambani,

Amesema bundi huyo ana uwezo wa kula panya zaidi ya 12 kwa usiku mmoja hivyo hakuna sababu ya kumchukia na kuwataka wale wote wenye dhana potofu na kumuona bundi kama mnyama mbaya mwenye kuleta mikosi kuachana na dhana hiyo badala yake wamuone kuwa ni rafiki mzuri wa wakulima kwani ana uwezo mkubwa wa kuwakomboa wakulima dhidi ya panya waharibifu wa mashambani.

                                

“Sisi tunamuita bundi kama rafiki wa mkulima, jinsi ya kumpata utatakiwa kuandaa  kihota chako vizuri kwa ajili ya kumvutia bundi, hapo bundi ana uwezo wa kuja na kuingia katika kihota hicho na kuweza kukaa na kudhibiti panya waliopo katika shamba lako, hivyo hatuna sababu ya kumuogopa wala kumuhofia”, amesema Mtafiti huyo.

Amesema ni vizuri kutumia teknolojia hiyo ambayo kazi yake ni kuandaa kihota tu ambacho kitamuwezesha bundi huyo kukaa na kwamba teknolojia hiyo ina faida zaidi ukilinganisha na matumizi ya sumu za kuua panya ambazo usipofuata maelekezo vizuri unaweza kuleta madhara katika afya za binadamu.

 






Post a Comment

0 Comments