SUAMEDIA

SUA kushirikiana na Halmashauri ya Mpimbwe kutoa elimu na tafiti kwa wakulima na wafugaji

 Na: Edson Kanisa - Katavi

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) na Halmashauri ya Wilaya ya Mpimbwe mkoani Katavi zimekubaliana kushirikiana kupitia vyombo vyake vya habari vya SUA Media na Mpimbwe FM katika kutoa elimu, teknolojia, ubunifu na matokeo ya utafiti katika sekta ya kilimo.

Halmashauri ya Wilaya ya Mpimbwe Bi. Shamim Mwariko akizungumza na ujumbe kutoka SUA (hauko pichani)

Akizungumza na ujumbe wa SUA uliofika ofisini kwake Julai 16, 2024 Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpimbwe Bi. Shamim Mwariko amesema wamefurahishwa na wazo hilo la SUA kwani ili kuleta maendeleo ya kilimo nchini ni muhimu wakajua mbinu bora za kilimo.

Amesema kupitia ushirikiano wa SUA na Halmashauri hiyo utasaidia kufikisha elimu, teknolojia, ubunifu na matokeo ya utafiti huku akisisitiza watafiti nchini wakiwemo wa SUA kutoa matokeo ya utafiti kwa lugha rahisi ambayo inaeleweka na mkulima.

Halmashauri ya Wilaya ya Mpimbwe Bi. Shamim Mwariko akizungumza na ujumbe kutoka SUA ulioongozwa na Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Masoko SUA Bi. Magobeko wa pili (kulia) wengine ni  Meneja wa Vipindi Mpimbwe FM Bw. Ally Chimela (kushoto) na wa kwanza (kulia) ni Afisa Mawasiliano Msaidizi SUA Bw. Edson Kanisa

Akizungumza wakati akitoa ombi la SUA kushirikiana na Halmashauri hiyo Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Masoko SUA Bi. Suzana Magobeko amesema Menejimenti ya SUA kupitia vikao vyake iliona ni muhimu kuunga mkono juhudi zilizofanywa na Halmashauri hiyo za kuwa na chombo cha habari Mpimbwe FM kwa kutoa maudhui yanayoweza kuwasaidia wakulima na wafugaji ili kuinua sekta hiyo nchini.

Muonekano wa studio za kisasa za Mpimbwe FM

Bi. Magobeko amesema SUA itahakikisha wataalam wake katika sekta ya kilimo wanashiriki kikamilifu katika kutoa habari na maudhui kupitia Mpimbwe FM na SUA Media pia itakuwa ikipokea na kutoa habari za Halmashauri hiyo kupitia vyombo vyake vya SUA FM na mitandao yake ya kijamii.

Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Masoko SUA Bi. Suzana Magobeko wa pili  (kulia) na Msimamizi wa SUA Media Bw. Gerald Lwomile wa pili (kushoto) wakiwa na Meneja wa Vipindi Mpimbwe FM Bw. Ally Chimela (kulia) na mtangazaji wa Mpimbwe FM Bw. Hamadi Mtambo (kushoto)


Post a Comment

0 Comments