SUAMEDIA

Wanasayansi wa Sayansi ya Misitu waliopikwa SUA watasaidia nchi zao - Prof. Kashaigili

Na: Gerald Lwomile

Imeelezwa kuwa Shahada ya Uzamivu ya Sayansi ya Misitu chini ya Mradi wa (REFOREST) inayotolewa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) ​​ni ya kipekee na itatoa wahitimu wabobevu katika sekta ya misitu na kusaidia kutunza na kulinda misitu hasa katika nchi zilizoko Kusini mwa Jangwa la Sahara.

Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Uzamili, Utafiti, na Uhaulishaji wa Teknolojia na Ushauri wa Kitaalamu Prof. Japhet Kashaigili aliyeketi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wahadhiri na Wafunzi wa Uzamivu (Picha zote na Mabula Mussa)

Haya yamesemwa Juni 13, 2024 na Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Uzamili, Utafiti, na Uhaulishaji wa Teknolojia na Ushauri wa Kitaalamu Prof. Japhet Kashaigili wakati akifungua warsha ya uwasilishaji wa matokeo ya utafiti kwa wanafunzi wa Shahada ya Uzamivu kutoka SUA.

Prof. Kashaigili amesema wanasayansi hao wabobevu katika sekta ya misitu pamoja na kupata mafunzo lakini pia wamefanya utafiti katika nchi zao na kuwa mbinu hiyo ililenga kuimarisha ubora na kuongeza idadi ya wanasayansi wenye uwezo wa kufanya utafiti na kuwezesha wahitimu katika ukanda wa Jangwa la Sahara kuwa na ushirikiano katika uhifadhi wa misitu.

Prof. Japhet Kashaigili akifungua warsha hiyo

Amesema warsha hizi za uwasilishaji wa matokeo ya utafiti hujenga daraja na kuwajengea uelewa wanasayansi na hata watunga sera wakati wa  kushughulikia masuala muhimu, kutoa na kusambaza maarifa mapya ili kuleta maendeleo kupitia matokeo ya utafiti.

Akizungumzia utafiti wake Bi. Jacquline Kajembe Mwanafunzi wa Shahada ya Uzamivu aliyefanya utafiti  wa kuangalia mnyororo wa thamani katika viungo amesema ili kuwa na uzalishaji mzuri wa viungo inahitajika misitu endelevu na ndiyo maana maana maeneo ya Amani wilayani Muheza mkoani Tanga na maeneo ya Milima ya Uluguru ambapo ndiko amefanyia utafiti wake yamekuwa na ufanisi mkubwa katika uzalishaji wa viungo na kuwa jitihada zinatakiwa kuoongezwa katika kuwaelimisha wakulima kuhakikisha wanalima kilimo cha kisasa pasipo kuharibu misitu.

Naye mwanafunzi kutoka Rwanda Bw. Elias Nelly Bapfakurera  amesema kuwa miti iliyopo kwenye kilimo mseto ina umuhimu mkubwa kwenye upatikanaji wa kuni za kupikia pamoja na kukabiliana na mabadiliko tabia nchi.

Kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi ili kufungua warsha hiyo Mratibu wa Mradi wa REFOREST Prof. Romanus Ishengoma amesema wanafunzi hao wa Shahada ya Uzamivu wamefanya utafiti katika nchi zao na wanatarajia matokeo hayo ya utafiti yatazinufaisha nchi zao na hasa katika nyororo mzima wa thamani wa ukuaji wa misitu.

 Mratibu wa Mradi wa REFOREST Prof. Romanus Ishengoma akizungumza katika warsha hiyo

Amesema wanafunzi kutoka nchi za Mozambique, Ethiopia, Uganda, Rwanda na Tanzania wamesoma na kusimamiwa vyema na wabobezi katika sekta ya misitu na kuwataka wanafunzi hao kuhakikisha wanafaulu na kuhakikisha tafiti zao zinachapishwa katika majarida makubwa ya kisayansi duniani ili zilete maendeleo katika nchi zao na Afrika kwa ujumla

Picha chini ni wanafunzi wa Shahada ya Uzamivu na wasimamizi wao 







Post a Comment

0 Comments