SUAMEDIA

SUA yasifika kwa kuzalisha wanafunzi bora kuendana na Soko la Ajira

 Na: Tatyana Celestine

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeendelea kupongezwa kwa kuzidi kuzalisha wanafunzi walio bora katika soko la ajira na kuonesha matokeo chanya katika kazi hivyo kufanya Sekta ya kilimo na viwanda kukua kwa kuzingatia ubora na kuwategemea wanafunzi hao kupelekea kukiwakilisha vema chuo hicho duniani na kutengeneza taswira kwamba wanahitajika katika maeneo mbalimbali ndani nje ya nchi.

                            

Hayo yamesemwa katika Kikao cha Kamati ya Ushauri wa Viwanda kilichojumuisha washiriki kutoka Taasisi na makampuni mbalimbali nchini pamoja na SUA lengo likiwa ni kupitia shughuli zilizofanywa na kitengo cha mashirikiano ya viwanda na kutoa ushauri  wa mpango kazi katika mwaka ujao ambacho kimefanikiwa kwa kujipambanua kuona wanawezaje kuwa mabalozi wa mabadiliko pamoja na kuchochea,  kuhamasisha urithi wa teknolojia mpya kwa kutumia njia mbalimbali kama majadiliano, na  vyombo vya habari.

                                 

Akizungumza na suamedia mara baada ya kikao hicho Mkurugenzi wa Mawasiliano Makampuni ya Bakhresa ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Ushauri wa Viwanda SUA Bw. Hussein Ally amesema kuwa wahitimu kutoka SUA wamekuwa wakifanya vizuri katika maeneo mbalimbali hii inaonesha wamepata mafunzo vizuri kwa kukabiliana na soko la ajira hivyo makampuni na maeneo mengine ya kazi nchini wameshauriwa kuwachukua wahitimu hao bila ukakasi wowote kutokana na uelewa, uwajibikaji pamoja na ujuzi wa teknolojia mpya.

                                

Aidha ameongeza kuwa makampuni ya Bakhresa yataendelea na utaratibu wa kuwapokea wahitimu katika mafunzo kwa vitendo kwani wao hawana hofu wala sababu ya kuficha teknolojia zao wanaamini wao kwa kufanya hivyo wanatoa mchango mkubwa katika kukuza vijana kikazi, sekta ya viwanda na kilimo kupitia utekelezaji wao kwa weledi na ufanisi.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kampuni ya Intermech Engeneering LTD, Mhandisi Petter Chisawillo  amesema kuwa wamekuwa na mahusiano na SUA kwa muda mrefu kupitia bidhaa mbalimbali ikiwemo, mihogo , kusambaza teknolojia za usindikaji wa mihogo vijijini pamoja na kuwapokea wanafunzi wa SUA kufanya mafunzo kwa vitendo kwani kwa kufanya hivyo inawasaidia wao kupata maarifa ambayo wasingeweza kuwanayo kama wangefanya wenyewe.

                           

Mhandisi huyo amesema kuna uhitaji wa wao kuzidisha ushirikiano wa pamoja katika kutatua changamoto zinazojitokeza hasa katika suala zima la teknolojia rahisi kwa ajili ya kuweka mitambo ya kusaidia kilimo kuanzia mashambani mpaka usindikaji wa bidhaa, kufanya ubunifu, utafiti na kuweka maarifa ili viwanda viweze kujua ni kitu gani kinaweza kusaidia vijijini kwa maana hiyo ni njia sahihi ya kuinua kilimo nchini.

                                   

Alipotakiwa kuzungumzia namna gani mkulima mdogo anaweza kunufaika kutokana na wao kuwa wajumbe katika kamati ya Ushauri wa Viwanda Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Mtandao wa Wakulima Wadogo Tanzania (MVIWATA) Bw. Stephen Ruvuga amesema lengo la kufanya tafiti na mipango katika sekta ya kilimo ni kuelekeza kwa mkulima mwenyewe hivyo kila kinachofanyika kinaakisi ndoto, maendeleo, malengo kwa mkulima sambamba  na wao kama chombo wameona kuna ombwe katika elimu inayotolewa vyuoni na mkulima mwenyewe hivyo kwa wao kutoa ushauri unaoakisi uhalisia kupitia kamati hiyo inaleta matumaini katika kutatua changamoto kwenye sekta ya kilimo na viwanda.

                         

Naye Naibu Mratibu wa Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mabadiliko ya Kiuchumi (HEET) SUA Dkt. Winfred Mbungu amesema Taasisi ya Elimu ya juu inatakiwa kuendana na mabadiliko ya Teknolojia pasi kuachwa nyuma na Tasnia hivyo kikao hicho kimelenga kusaidia wahitimu wa SUA kuweza kufaidika kwa namna mahitaji ya viwanda yanaweza kutekelezwa kupitia wahitimu wao kwani wao wanatakiwa kuzalisha wafanyakazi au waanzilishi wa viwanda na biashara ndio sababu kupitia mradi huo wamejitahidi kuhimarisha miundombinu ya ufundishaji kama vile karakana na maabara pamoja na kuboresha mashirikiano yao na sekta binafsi ili kutumia teknolojia zao.

                                  

Aidha kupitia kikao hicho SUA imeendelea kushauriwa kuzidi kutengeneza mashirikiano na makampuni mengine ikiwemo Bagamoyo Sugar ili kuongeza wigo katika kusaidia maendeleo ya viwanda katika kuzalisha wataalamu walio na weledi wa kutosha katika kila eneo linalohusu kilimo na uwekezaji na kwamba  itasadia kujua ni kwa namna gani wanaweza kutoa elimu hiyo katika ubora pamoja na kubaini teknolojia mpya ambazo zitarahisisha kukua kwa Uchumi wa nchi na sekta ya kilimo kwa ujumla.

                        



















PICHA ZAID BOFYA HAPA
https://tatyana35.pixieset.com/kikaochakamatiyaushauriwaviwanda/

                KATIKA VIDEO

                

Post a Comment

0 Comments