SUAMEDIA

Maabara ya Mageuzi ya CLARITY yatumika kutafiti upatikanaji wa maji ardhini

 Na: Farida Mkongwe

Imeelezwa kuwa Maabara ya Mageuzi iliyopo chini ya Mradi wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi na Ustahimilivu katika Nyanda Kavu za Kitropiki (CLARITY) ambayo inashirikisha wadau mbalimbali wanaotafuta suluhisho za changamoto ya mabadiliko ya tabianchi na athari zake katika upatikanaji wa maji ya ardhini inaweza kusaidia  kutatua changamoto ya upatikanaji wa maji jijini Dodoma.

                                         

Hayo yameelezwa na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaalam, Prof. Maulid Mwatawala wakati akizungumza na waandishi wa habari katika  Warsha ya Maabara ya Mabadiliko iliyofanyika jijini Dodoma.

 Prof. Mwatawala amesema changamoto ya upatikanaji wa maji jijini Dodoma ni ya muda mrefu kutokana na jiji hilo kuwa katika eneo ambalo ni nyanda kavu na ndiyo sababu mradi wa CLARITY uliona umuhimu wa kufanya utafiti wa kuangalia maji yaliyopo ardhini namna ya kuyatunza, kuyasambaza kwa upatikanaji ambao utakuwa wa kiusawa kwa jinsia zote na makundi yote na pia uwe ni endelevu na wa uhakika.

                                        

 “Kundi hili imekaa hapa kuangalia nini utakuwa mchango wa maji yaliyopo ardhini katika kutatua changamoto ya upatikanaji wa maji hapa Dodoma ikihusisha pia vyanzo vingine, sasa wadau hawa wamekutana ili kutoa suluhisho la pamoja, jambo mojawapo tunaloliangalia kwa sasa ili tuweza kwenda mbele ni lazima tutunze vyanzo vya maji vilivyopo na ambalo wanalizungumzia wadau hapa ni upandaji wa miti na kuitunza kwa sababu miti ikipandwa isipotunzwa inapotea”, amesema Prof. Mwatawala.

                                       

 Kwa upande wake Mkuu wa Mradi huo na Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Uzamili, Utafiti, Uhaulishaji wa Teknolojia na Ushauri wa Kitaalamu SUA Prof. Japhet Kashaigili amesema Maabara ya Mageuzi ya CLARITY mjini Dodoma inaongozwa na SUA huku akibainisha kuwa CLARITY imelenga kuongeza usawa, uendelevu na ustahimilivu wa njia za maji za tabianchi katika maeneo kavu ya kitropiki na kuyaingiza masuluhisho yatakayopatikana katika michakato ya kisera na utekelezaji wa kijumuiya.                                                                                                                         

                                    

 Naye Mtaalamu wa Maji chini ya Ardhi kutoka Bonde la Maji la Wami Ruvu Ezra Mwakabumbe amesema katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi wao wamepanda miti 17,600 kwa mwaka huu na kutoa hamasa kwa watu mbalimbali kuendelea kupanda miti na kuhifadhi vyanzo vya maji.

                                    

 “Pia tumeunda jumuiya za watumiaji maji ambazo zimekuwa na msaada mkubwa kwetu kuweza kutupatia taarifa za watu wanaovamia vyanzo vya maji lakini pia tumeingia makubaliano na JKT Makutupora kufanya doria mara kwa mara kwenye ile hifadhi ya maji ili kudhibiti mifugo na shughuli za kibinadamu zisiweze kufanyika ndani ya hifadhi ya maji”, amesema mtaalamu huyo.

                                                        

 Mradi wa CLARITY ambao ni wa miaka mitatu na miezi sita ulianza mwaka 2023  na unafadhiliwa na Kituo cha Utafiti wa Maendeleo ya Kimataifa (IDRC Canada), Ofisi ya Mambo ya Nje, Jumuiya ya Madola na Maendeleo (FCDO, Uingereza)  chini ya mpango wa Kukabiliana na Hali ya Hewa na Ustahimilivu (CLARE).

 

                                 

   












Picha na Video: Tatyana Celestine

BOFYA LINK HAPO CHINI KUTAZAMA PICHA ZAIDI 

Post a Comment

0 Comments