SUAMEDIA

Watanzania watakiwa kutunza mazingira ili kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi

 

Na: Farida Mkongwe

Watanzania wametakiwa kuhakikisha wanatunza mazingira yanayowazunguka kwa hali na mali ili kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ambayo yameonekana kuleta athari kubwa katika jamii na taifa kwa ujumla.



Wito huo umetolewa Mei 28, 2024 na Bi. Mwanasha Tumbo kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais ambaye pia ni Mratibu wa masuala ya Biashara ya Kaboni wakati akizungumza na SUA Media kuhusu Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani ambayo kitaifa yatafanyika jijini Dodoma Juni 5, 2024.

Bi Mwanasha amesema lengo kubwa la maadhimisho hayo ni kuhamasisha na kukumbushana faida zitokanazo na utunzaji na uhifadhi wa mazingira  sanjari na kuelezana athari za uharibifu wa mazingira ambao umesababisha mabadiliko ya tabianchi.

“Mabadiliko haya ya tabianchi yametuletea mvua tusizotarajia tumeona mafuriko tusiyoyoyategemea, watu wanakufa, mazao yanaharibika mashambani, mabadiliko haya yametuletea vimbunga mpaka vinaitwa kina Hidaya, sasa tunatakiwa kukabiliana na athari hizo ikiwa ni pamoja na kutunza mazingira yetu na kuzuia kuzalisha gesi joto”, amesema Mratibu huyo.

Amesema shughuli mbalimbali zitafanyika katika Maadhimisho ya Wiki ya Mazingira Duniani ikiwa ni pamoja na kampeni ya usafi wa mazingira Kitaifa ambayo itafanyika Juni Mosi, 2024 katika maeneo mbalimbali nchini na kuwataka wananchi kushiriki ipasavyo katika kampeni hiyo.

Maadhimisho hayo ambayo kitaifa yatafanyika jijini Dodoma yamebeba kauli mbiu isemayo “Urejeshwaji wa Ardhi, Ustahamilivu wa Hali ya Jangwa na Ukame ” ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

KATIKA VIDEO

Post a Comment

0 Comments