Na: Siwema Malibiche
Waandishi
wa habari wameaswa kuendelea kushiriki katika utunzaji wa mazingira hasa
upandaji wa miti katika vyanzo vya maji
ili kusaidia kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi kwa ajili ya vizazi vilivyopo na vijavyo.
Rai hiyo imetolewa na Katibu Mtendaji wa Chama cha Waandishi wa Habari mkoa wa Morogoro (MOROPC) Bi. Liliani Lucas Kasenene wakati wa zoezi la upandaji miti ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari mkoani hapo ambapo wanahabari wamepanda miti zaidi ya 150 pembezoni mwa mto Lukulunge uliopo kata ya Mzinga kwa lengo la kuendelea kutunza vyanzo vya maji.
Bi. Liliani amesema mwaka huu MOROPC imeamua kuadhimisha siku hiyo kwa kupanda miti ili kuendana na Kauli Mbiu ya Maadhimisho hayo kitaifa kwa mwaka 2024 iliyosema “Waandishi wa Habari na Mabadiliko ya Tabianchi”.
Aidha
amesema kuwa wanahabari wana nafasi kubwa ya kuielimisha jamii katika suala la utunzaji
wa mazingira huku akisisitiza kuwa
suala la upandaji miti litakuwa ni jambo endelevu kwa waandishi hao.
Kwa upande wake Pato Haule Mtumishi
kutoka Bonde la Wami Ruvu mkoani Morogoro amewapongeza waandishi wa
habari walioshiriki katika zoezi la upandaji wa miti na amesema kama Bodi
itaendelea kushirikiana nao ili wananchi waendelee kupata maji safi na ya
uhakika ili kuendeleza shughuli nyingine za kiuchumi.
Pia
amewataka wakazi wote wanaoendesha shughuli zao za kiuchumi kando ya mito kuacha shughuli
hizo huku akiahidi kuwa wataendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa
kuhifadhi na kutunza vyanzo vya maji.
Naye Mwenyekiti wa Kikundi
cha Wahamasishaji Tanzania wanaofanya kazi chini ya Bonde la Wami
Ruvu iliyoko chini ya Wizara ya Maji Abubakari Miraji Sisango amewapongeza waandishi wa habari kwa kuamua
kushiriki katika upandaji wa miti na ametoa wito kwa wakazi wote walioko
karibu na vyanzo vya maji kutunza vyanzo hivyo kwa manufaa ya vizazi vijavyo
huku akisisitiza kuwa kila tone la maji nchini linapaswa kuhifadhiwa.
Baadhi ya Waandishi wa habari walioshiriki zoezi hilo la upandaji miti akiwemo Bibi. Elizabeth Tanzania wamesema
ni jambo zuri kwa waandishi kushiriki
katika upandaji wa miti ili kusaidia harakati za kupambana na mabadiliko ya tabia nchi kwa sababu mazingira yanapoharibika
waathirika wake ni jamii yote kwa ujumla wakiwemo wanahabari.
Kassim Abdul Chunga mkazi wa
kata ya Mzinga amewashukuru wanahabari wote waliojitokeza katika
upandaji wa miti karibu na mto huo na amekiri kuwa
wamekuwa wanapatiwa elimu ya kutunza mazingira mara kwa mara na hivyo
kuwataka wanajamii wenzake kuzingatia maelekezo wanayopewa na wataalam wa
mazingira.
0 Comments