SUAMEDIA

Balozi wa Ubelgiji nchini Tanzania amesifu kazi inayofanywa na Watafiti wa SUA

 

Na, Winfrida Nicolaus

Balozi wa Ubelgiji nchini Tanzania Mhe. Peter HuygheBaert amesifu na kuridhishwa na kazi inayofanywa na Watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) pamoja na Kituo cha Utafiti cha Mradi wa Apopo katika kuhakikisha wanatatua changamoto mbalimbali kwenye jamii ya Kitanzania ikiwemo kuwatumia panya katika utatuzi wa magonjwa kama vile Kifua Kikuu (TB)

                                    

Akizungumza na SUA Media Balozi huyo amesema kufanya kazi na SUA inamaanisha wanafanya kazi na nchi nzima ya Tanzania hivyo ushirikiano uliopo baina ya nchi hizo mbili ni wa manufaa makubwa na wakiwa kama wafadhili wakubwa wa Mradi wa APOPO inaleta hamasa na kufurahisha kuona ushirikiano huo unafanya kazi nzuri katika utatuzi wa changamoto mbalimbali.

“Kile tulichokiona kinavutia sana kutokana na ushirikiano uliopo kwanza kabisa baina ya SUA na Chuo chetu cha Antwerp na baadaye kushirikiana katika Mradi ambao unavutia sana wa kutumia Panya katika matumizi mbalimbali lengo likiwa kuifanya jamii kuwa salama”, amesema Balozi huyo

Kwa upande wake Mhadhiri kutoka SUA Prof. Abdul Katakweba akimwakilisha Prof. Allen Malisa Mkurugenzi wa Taasisi ya Kudhibiti Viumbe Hai Waharibifu amesema APOPO inafanya kazi chini ya Taasisi ya SUA lakini pia kuna ushirikiano baina ya SUA, APOPO pamoja na Chuo Kikuu cha Antwerp kilichopo nchini Ubelgiji.

Amesema APOPO ni Taasisi isiyo ya Kiserikali kutoka nchini Ubelgiji na huo ubalozi ndio unaofadhili sehemu kubwa katika tafiti zinazofanywa na Taasisi hiyo pamoja na SUA hivyo ujio wa balozi huyo ni kujiridhisha kwa kuangalia endapo misaada inayotolewa na nchi yao kama inafanya kazi vizuri au lah! na kitu kizuri ni kuwa kazi imeonekana.

“Ushirikiano wetu mkubwa kati ya APOPO na SUA ni ufanyaji wa Tafiti katika kusaidia binadamu kwa ndani ya nchi na nje ya Tanzania ambapo tunatumia panya kunusa mabomu lakini pia makohozi kwa ajili ya kubaini vimelea vya Kifua kikuu na kwa upande wa Tanzania tafiti hiyo imekwenda vizuri sana ambapo tuna hospitali zaidi ya 58 ambazo  panya hao wanaweza kutumia makohozi ili kuweza kubaini vimelea hivyo”, amesema Prof. Katakweba

Katika Ziara hiyo Balozi huyo ametembelea maeneo mbalimbali ikiwemo Maabara ya kutambua vimelea vya Kifua Kikuu (Morogoro TB Detection), Shamba la Mfano la Mafunzo la Kilimo Msitu, Eneo la Mafunzo ya Panya wanaokabiliana na majanga ikiwemo kutegua mabomu na baadaye Ofisi ya Makamu wa Mkuu wa Chuo cha SUA.

 










Post a Comment

0 Comments