SUAMEDIA

Kazi za wabunifu nchini zina matokeo chanya - Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.

 Na: Gerald Lwomile

Serikali imesema kazi nyingi za wabunifu nchini zina matokeo chanya jambo ambalo litalisadia taifa kuhakikisha linasonga mbele na kutatua changamoto mbalimbali.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa akizungumza katika kilele cha Madhimisho ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu (Picha zote na Gerald Lwomile)

Hayo yamesemwa Mei 31, 2024 na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa wakati akiahirisha Maadhimisho ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu iliyofanyika jijini Tanga.

Mhe. Majaliwa amesema ameshuhudia ubunifu wa hali juu katika wiki hiyo ikiwemo vijana watafiti mbalimbali ambao wamekuja na teknolojia na ubunifu mbalimbali ambao utasaidia taifa kutoagiza vifaa nje na kutumia fedha nyingi za kigeni.

“Nimeona kijana mmoja kutoka VETA ametengeneza chombo kinachokuza sauti na kumuwezesha mwenzetu ambaye hasikii vizuri, mwenye usikivu hafifu kusikia vizuri, sasa kama unaweza kutengeneza ukabuni chombo kama hiki na huku tukitambua kuna watanzania wana matatizo ya kusikia tayari umeshapata soko” amesema Mhe, Majaliwa.

Timu ya maonesho ya SUA iliyoshiriki katika wiki hiyo, walikaa katikati na Makamu Mkuu wa Chuo Prof. Chibunda, kushoto na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaalamu Prof. Maulid Mwatawala na kulia ni Dkt. Devota Kilave Mkurugenzi ICE

Akielezea mipango ya Serikali katika kukuza utafiti, ujuzi na ubunifu Waziri Mkuu Mhe. Majaliwa amesema Serikali itaendelea kuweka nguvu katika eneo hilo ili lilete tija nchini.

Akizungumza kabla ya kumkaribisha Waziri Mkuu, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof. Adolf Mkenda ameishukuru Serikali kwa kutoa ufadhili wa masomo kwa wanafunzi wote wanaosoma masomo ya Sayansi.

Prof. Mkenda amesema ufadhili huo utachochea na kutoa hamasa kwa vijana wengi kusoma masomo ya Sayansi, Uhandisi, Elimu Tiba, Hisabati na TEHAMA.

Wakati huo huo Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imetoa zawadi na vyeti kwa watafiti mbalimbali ambao wametoa machapashio yao na kufanya vizuri kwenye majarida makubwa ya kisayansi duniani.

Miongoni mwao ni Marehemu Prof. Ludovick Kazwala kutoka SUA ambaye zawadi yake na cheti kilipokewa na familia yake ikiongozwa na mkewe Bi. Lydia Kazwala, mwingine ni Prof. Hezron Nonga kutoka Ndaki ya Tiba ya Wanyama na Sayansi Shirikishi.

Mke wa Marehemu Prof. Kazwala Bi. Lidya Kazwala akipokea cheti kutoka kwa Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa.

Maadhimisho ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yalianza Mei 25, 2024 na kufikia kilele Mei 31, 2024, maadhimisho hayo yalibebwa na kauli mbiu isemayo ‘Elimu, Ujuzi na Ubunifu kwa Uchumi Shindani’

Prof. Nonga akipokea cheti kutoka kwa Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa.


Post a Comment

0 Comments