SUAMEDIA

WFP na SUA kushirikiana kuhakikisha kunakuwa na usalama wa chakula

 Na: Gerald Lwomile

Shirika la Mpango wa Chakula duniani ukanda wa Tanzania (WFP) na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) wamesaini Mkataba wa Ushirikiano ambao utasaidia tafiti, matumizi ya teknolojia ikiwemo Akiri Mnemba na namna ya kukabiliana na Mabadiliko ya Tabia Nchi.

Mwakilishi wa WFP nchini Tanzania Bi. Sarah Gordon-Gibson (kushoto) akibadilishana Mkataba wa Ushirikiano na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Prof. Raphael Chibunda (Picha zote na Gerald Lwomile)

Akizungumza Aprili 2, 2024 wakati wa utiaji saini makubaliano hayo Mwakilishi wa WFP nchini Tanzania Bi. Sarah Gordon-Gibson amesema mbali na maeneo hayo lakini pia Mkataba huo wa Ushirikiano utagusa maeneo mengine kama kubadilishana ujuzi na kuwajengea uwezo watafiti wa namna ya kutafuta fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali.

Amesema WFP imetenga zaidi ya Dola za Marekeni elfu 60 ambazo ni sawa na zaidi ya shilingi Milioni 150  za Tanzania kwa ajili ya SUA na wanaamini kuwa tafiti na uvumbuzi katika sekta ya kilimo na chakula ni kichocheo kikubwa cha mabadiliko katika sekta hiyo.

Mwakilishi wa WFP nchini Tanzania Bi. Sarah Gordon-Gibson akizungumza baada ya kusaini Mkataba wa Usirikiano na SUA

Bi. Sarah amesema ushirikiano baina ya SUA na WFP umekuja wakati mwafaka kwani utarahisisha na kuzipa msukumo tafiti za kisayansi, ameongeza kuwa kulingana na mpango mkakati wa WFP wa mwaka 2022 hadi 2027 na Ajenda ya Maendeleo Endelevu hadi ifikapo 2030,  uvumbuzi uwe kielelezo muhimu cha kuhakikisha usalama wa chakula na lishe kwa watu wote.

Akizungumzia ushirikiano kati ya WFP na SUA, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Prof. Raphael Chibunda amesema SUA imefurahishwa na ushirikiano huo kwani utaongeza thamani katika maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na utafiti, uvumbuzi na teknolojia za kilimo.

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Prof. Raphael Chibunda (kushoto) akifurahia jambo na Mwakilishi wa WFP nchini Tanzania Bi. Sarah Gordon-Gibson

Prof. Chibunda amesema katika kuhakikisha ushirikiano huo unakuwa imara SUA itafanya kazi bega kwa bega na WFP ili kuhakikisha inawasaidia wanataaluma, watafiti na wakulima kwa ujumla katika kuhakikisha usalama wa chakula na lishe.

Naye Mratibu wa Teknolojia na Ushauri wa Kitaalam SUA Dkt. Doreen Ndosi amesema ushirikiano huo wa WFP na SUA utatimiza ndoto ya Chuo hicho kuhakikisha usalama wa chakula kuanzia shambani, mavuno, uhifadhi, usafirishwaji kwa usalama na kumfikia mlaji wa mwisho kikiwa salama.

Mratibu wa Teknolojia na Ushauri wa Kitaalam SUA Dkt. Doreen Ndosi (aliyesimama) akielezea manufaa ya ushirikiano huo

Amesema tayari kuna miradi kadhaa ambayo wataalamu wa SUA wameanza kushauriana na WFP ambayo itaangalia miradi hiyo ili kumsaidia mkulima kufanya kilimo cha kisasa kuanzia mkulima mdogo, wa kati na mkulima mkubwa kutumia njia za kisasa na kupata tija katika kilimo.

Picha chini ni matukio mbalimbali wakati na baada ya kuweka saini Mkataba wa Ushirikiano 👇













Post a Comment

0 Comments