SUAMEDIA

Viongozi SUA watakiwa kutimiza majukumu yao ili kufanikisha malengo ya Chuo

 

Na: Farida Mkongwe

Viongozi wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) wametakiwa kuwa na nia thabiti ya kutekeleza kazi zao ili majukumu ambayo Chuo kimekabidhiwa na Serikali ya kuwa ni Chuo cha Kilimo yafanikiwe kwa ufanisi na kutimiza ndoto za Serikali katika Sekta ya Kilimo nchini.

Makamu Mkuu wa Chuo cha SUA Prof. Raphael Chibunda akizungumza wakati akifungua mafunzo ya uongozi kwa Viongozi wa SUA yanayofanyika mjini Morogoro (Picha na Mabula Musa)


Wito huo umetolewa Aprili 2, 2024 na Makamu Mkuu wa Chuo hicho Prof. Raphael Chibunda wakati akifungua mafunzo ya uongozi kwa Viongozi wa SUA yanayofanyika mjini Morogoro ambapo amesema kuwa nafasi ya Chuo hicho katika maendeleo ya Taifa ni kubwa na hivyo viongozi wana dhamana ya kuhakikisha wanafanikisha malengo hayo.

Prof. Chibunda amesema ni wajibu wa viongozi kuzingatia miiko ya falsafa za uwajibikaji unaozingatia maadili ya Uadilifu, kutii Miongozo, Kanuni na Sheria za nchi na hivyo kuwa mifano bora kwa Wataalam na Viongozi wanaowaandaa na kuwapa mafunzo ya utaaalam wakiwemo wanafunzi wa Chuo hicho.

“Wito wangu kwetu sote ni kubadilisha kabisa mfumo wetu wa kusimamia utekelezaji wa majukumu ya Chuo chetu kwa mazoea na kuingia katika falsafa halisi ya usimamizi wa kupata matokeo chanya yenye utendaji kazi wa vipimo vya matokeo ya kila siku kwa kila Mtumishi tunayemsimamia”, amesema Prof. Chibunda.

Katika mafunzo hayo ya siku tatu Viongozi wa SUA watajifunza kuhusu Kanuni za Maadili ya Utumishi wa Umma, Akili ya Kihisia katika Uongozi, Afya ya akili pamoja na Nafasi za Viongozi katika Michakato ya Kushughulikia Masuala ya Kinidhamu kwa Watumishi.

Mafunzo mengine yatakayotolewa ni kuhusu Ukarimu na Uzingatiwaji wa Itifaki katika Utumishi wa Umma, Ujuzi wa Uongozi na Usimamizi, Utunzaji wa Siri za Ofisi katika Utumishi wa Umma na Uadilifu mahala pa kazi. 






Post a Comment

0 Comments