SUAMEDIA

Watumishi wa Umma watakiwa kuzingatia Maadili ya kazi zao

 

Na: Farida Mkongwe

Viongozi na watumishi wa umma wametakiwa kuzingatia na kulipa kipaumbele suala la maadili ili kutengeneza misingi imara ya utendaji kazi itakayoleta mafanikio katika Taasisi za Umma na Taifa kwa ujumla.


Katibu Msaidizi kutoka Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Makao Makuu, Bw. Fabian Pokella  wakati akiwasilisha makala kuhusu Kanuni za Maadili ya Utumishi wa Umma katika mafunzo ya uongozi kwa Viongozi wa SUA (Picha na mabula Musa)


Wito huo umetolewa Aprili 2, 2024 na Katibu Msaidizi kutoka Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Makao Makuu, Bw. Fabian Pokella  wakati akiwasilisha makala kuhusu Kanuni za Maadili ya Utumishi wa Umma katika mafunzo ya uongozi kwa Viongozi wa SUA yanayofanyika mjini Morogoro.

Bw. Pokella amesema suala la uadilifu linapaswa lijengwe katika mifumo yote kuanzia ngazi za familia ili kuzalisha viongozi wenye uadilifu lakini kwa upande wa Taasisi viongozi wanatakiwa kuwa mfano wa kuigwa kwa wanaowaongoza na kuwalea wakiwemo wanafunzi na hivyo kuzalisha viongozi waadilifu watakaoleta maendeleo ya Taifa.

“Pale ambapo viongozi hawatakuwa waadilifu kwanza kabisa wataathiri maendeleo ya nchi yetu lakini pia wanaweza kuchukuliwa hatua kwa mfano kiongozi asipokuwa muadilifu na kusababisha matumizi mabaya ya fedha za Serikali ambazo ni mali ya umma lazima sheria itachukua mkondo wake”, amesema Bw. Pokella.

Kwa upande wao baadhi ya viongozi wanaoshiriki mafunzo hayo akiwemo Prof. Agnes Sirima, Rasi wa Ndaki ya Misitu, Wanyamapori na Utalii kutoka SUA Kampasi ya Edward Moringe na Prof. Anna Sikira ambaye ni Naibu Rasi wa Ndaki upande wa Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaaluma Kampasi ya Mizengo Pinda, wameishukuru Menejimenti ya SUA kwa kuandaa mafunzo hayo ambayo yatawasaidia kutekeleza majukumu yao.

“Ni mafunzo muhimu kwetu sisi viongozi kwani yanatupa nyenzo muhimu ya kuitumia katika kutekeleza majukumu yetu, yanatuwezesha kujua na kuheshimu mamlaka za kiuongozi na kutambua mipaka yetu na tunaowaongoza, kwa kweli tunaishukuru sana Menejimenti ya SUA kwa mafunzo haya”, amesema Prof. Sirima.

“Nimegundua kwamba maadili ni kitu muhimu sana kwa Mtumishi yeyote yule lakini pia kuna Sheria za kiutumishi tunapaswa kuzifuata ili ziweze kutusaidia lakini kutujengea mahusiano mazuri kwetu sisi watumishi na viongozi kwa ujumla hali ambayo itatusaidia kutekeleza majukumu yetu ya kikazi na kuijenga nchi yetu ”, amesema Prof. Sikira.








Post a Comment

0 Comments