SUAMEDIA

SUA yafanikiwa kuhamasisha ufugaji wa samaki wilayani Kilombero

 

Na: Ayoub Mwigune

Katika kuhakikisha Afya za Watanzania zinaimarika kwa kula vyakula vya aina mbalimbali ikiwemo Samaki ambao ni kati ya vyakula muhimu vyenye protini, Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia Mradi wa Chakula, Kilimo na Lishe (FoodLAND) kimefanya uhamasishaji kwa wananchi wilayani Kilombero mkoani Morogoro kuweza kufuga Samaki kwa ajili ya kupata kitoweo zaidi ili kuongeza uimarishaji wa afya zao.




Akizungumza na SUA Media wilayani Kilombero mkoani Morogoro Mratibu wa Mradi wa FoodLAND Prof. Suzan Msolla amesema tafiti zilizofanyika zinaonesha kuwa pamoja na watu kuwa wanakula vyakula vya aina mbalimbali lakini ulaji wa vyakula vyenye protini ni mdogo sana kwa watanzania walio wengi hasa sehemu za vijijini na ndiyo maana wameona wahamasishe watu kuweza kufuga Samaki kwa tija.

“Kitu tulichokifanya huku tumekuwa na wakulima mbalimbali wanaopendelea kufuga Samaki ambao tuliwatambua kwanza na tuliwapatia Mafunzo mbalimbali ikiwemo namna ya kutengeneza mabwawa ya samaki ambayo yanakidhi mahitaji ya ufugaji wa Samaki na wale waliopenda kufuga samaki walitengeneza mabwawa yao wenyewe kwa gharama zao na sisi tulichokifanya ni kuwaletea vifaranga vya samaki”, amesema Prof. Msolla.

Prof. Msolla amesema wakulima baada ya kupandikiza vifaranga vya samaki walivyowapatia wameweza kukuza samaki hao kwa muda wa miezi nane hivyo zoezi ambalo limeendelea kwa sasa ni kuvua Samaki hao ambao wamefugwa kitaalamu na idadi yao kuwa kubwa na wenye umbo linalotakiwa ambapo imewasaidia wakulima hao kuwaingizia kipato na wengine kuwatumia kama kitoweo.

Ameongeza kuwa wao kama SUA kupitia Mradi wa FoodLAND wamefurahishwa sana kutokana na lengo lao la uhamasishaji wa ufugaji Samaki kutimia na kuleta hamasa kubwa sana kwa watu wengine kutaka kujihusisha na ukulima wa uzalishaji wa Samaki hivyo wana matarajio makubwa kuwa elimu hiyo ya ufugaji wa samaki itaenea katika maeneo mbalimbali nchini kwa kuwa wameshapokea maombi kutoka kwa watu mbalimbali wanaohitaji mafunzo ili waweze kufuga samaki kwa tija.

Kwa upande wake Dkt. Renalda Munubi kutoka SUA amesema Mafunzo yaliyoendana na vitendo waliyoyatoa kwa wakulima hao ambao wameweza kufuga samaki na kuwavuna yamewawezesha kutambua kuwa wanaweza kutotegemea samaki kutoka kwenye mito pekee na badala yake wanaweza kuwafuga wenyewe na kuwawezesha kuwapatia kipato cha kutosha lakini pia kuwatumia kama kitoweo kwa ajili ya kuboresha Afya zao.

Naye Festo Liguduliaka mkazi wa Kijiji cha Mshikamano kata ya Mang’ula B Halmashauri ya Ifakara mkoani Morogoro ambaye ni mfugaji wa samaki amesema Mradi wa FoodLAND umewawezesha kuona matokeo chanya kwenye suala zima la ufugaji wa samaki ambapo walijaribu mara nyingi kufuga lakini bila mafaniko hivyo Mradi huo umewafanya kutambua kuwa kila kitu kina utaratibu wake na ukifuata maelekezo kutoka kwa wataalam mafanikio yanakuja yenyewe.












Post a Comment

0 Comments