SUAMEDIA

Uongozi ni dhamana, viongozi tekelezeni maagizio ya Serikali - Rais Samia

 Na Gerald Lwomile

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amewataka viongozi na wananchi kuendelea kumuenzi Hayati Edward Moringe Sokoine kwa uwajibikaji na kufahamu kuwa uongozi ni dhamana.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia katika Kumbukiza ya miaka 40 ya Kifo cha aliyekuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Edward Moringe Sokoine (Picha zote na Gerald Lwomile)

Rais Samia amesema hayo Aprili 12, 2024 wakati akihutubia katika Misa ya Kumbukizi ya miaka 40 ya Kifo cha aliyekuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Edward Moringe Sokoine iliyofanyika wilayani Monduli mkoani Arusha.

“Tunatakiwa kuwa wafuatiliaji wa karibu maagizo yote yanayotolewa na Serikali ndani ya dhamana zetu, kama viongozi tunatakiwa kutekeleza maagizo yote yaliyotolewa na serikali na kuhakikisha yanatekelezwa” amesema Rais Samia

Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema, Hayati Sokoine alisimamia vyema operesheni mbalimbali ikiwemo Operesheni Uhujumu Uchumi na alisimamia bila woga pamoja na kuwepo kwa changamoto  mbalimbali.

Wake wa Viongozi Wastaafu (waliokaa mbele) wakiwa katika Misa ya Kumbukizi ya Hayati Edward Moringe Sokoine

Akizungumzia hali ya mafuriko inayoendelea nchini Rais Samia amewataka wananchi kuchukua tahadhari na kuondoka maeneo yenye mafuriko huku akiwataka viongozi kuhakikisha wanawasaidia wananchi katika maeneo hayo.

Kabla ya Rais Samia kukaribishwa kuhutubia katika Kumbukizi hiyo Mkuu wa Mkoa wa Arusha Paul Makonda amesema wananchi wa mkoa wa Arusha wana matumaini makubwa na Rais Samia.

Amesema miradi mbalimbali katika Sekta za Afya, Elimu na Miundombinu imeendelea kutekelezwa katika mkoa huo na kuongeza kuwa viongozi wa mkoa wa Arusha wameendelea na vikao mbalimbali kuhakikisha mkoa wa Arusha unakuwa mkoa wa kitalii hasa.

Akizungumza katika misa hiyo Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbu Kuu la Arusha Baba Askofu Isack Amani amesema hali ya ubaguzi, uonevu na majivuno kwa baadhi ya viongozi umeleta athari kubwa kwa watanzania.

Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbu Kuu la Arusha Baba Askofu Isack Amani akiongoza Misa ya Kumbukizi ya miaka 40 ya Kifo cha Hayati Sokoine

Amesema Hayati Sokoine alichukia rushwa na alikemea kwa nguvu zote maovu.

“Leo hii angekuwa hai angetwambia tujihadhari sana na Jani la Arusha, haiwezekani tukawa wastaarabu tusipojitenga na mambo maovu” amesema Askofu Isack Amani.

Kumbukizi ya miaka 40 ya Kifo cha Hayati Sokoine imehudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Makamu wa Rais Mhe. Dkt. Philipo Mpango, Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaaliwa, Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne Mhe. Jakaya Kikwete na wake wa viongozi mbalimbali wastaafu.

Picha chini ni viongozi mbalimbali wakiwemo wa kitaifa, taasisi na wananchi walioshiriki katika misa hiyo





Post a Comment

0 Comments