SUAMEDIA

Hayati Sokoine alikuwa ni Kiongozi aliyeandaliwa – Jaji Mstaafu Warioba

 Na: Farida Mkongwe

Makamu wa Rais na Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba amesema Hayati Edward Moringe Sokoine alikuwa ni Kiongozi aliyeandaliwa vizuri na jamii yake ya Kimaasai pamoja na Chama cha TANU ndiyo maana alikuwa Kiongozi mwenye kusimamia ukweli wakati wote.

                     

Mhe. Jaji Warioba ambaye pia ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) ameyasema hayo wakati akitoa mada  ya Sokoine: Kilimo na Maendeleo  kwenye Mdahalo wa Kitaifa wa Kumbukizi ya miaka 40 ya Hayati Edward Moringe Sokoine iliyofanyika chuoni hapo katika Kampasi ya Edward Moringe mjini Morogoro.

“Sokoine aliandaliwa kuwa mwaminifu kwa nchi yake, aliandaliwa kuwa na nidhamu na mchapa kazi, alikuwa Kiongozi mfuatiliaji na aliamini kiongozi ni lazima kwa imani yake uwe na uwezo wa kufanya kazi uliyopewa kama unaona huna uwezo wa kufanya hiyo kazi usikubali na alionesha kwa mfano pale alipokataa kuzitumikia baadhi ya nyidhifa alizopewa, sijui ni wangapi wanaweza kupata nafasi hiyo wakakataa”, amesema Jaji Mstaafu Warioba.

Viongozi wengine waliotoa mada katika mdahalo huo ni Spika wa Bunge Mstaafu Mhe. Anna Makinda, Profesa Mstaafu wa Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam Prof. Issa Shivji na Prof. Kalunde Sibuga kutoka SUA ambao wote walizungumzia uadilifu na uwajibikaji wa Hayati Sokoine.

“Mimi nimefanya naye kazi kwa mwaka mmoja tu lakini kikubwa tunachojifunza kwake ni nidhamu ya kazi na pili uadilifu alikuwa hayupo tayari kupokea zawadi na alikuwa mfuatiliaji wa mtu mmoja mmoja na pia alikuwa anasali sana”, amesema Mhe. Anna Makinda.

“Sokoine katika hotuba zake alikuwa akirudia rudia mambo matatu ambayo ni Taifa kujitosheleza kwa chakula ili nchi iweze kujikomboa na kuulinda uhuru wake, kujitegemea kwa nchi na kujenga na kukuza soko la ndani ambapo dhana hizi zote kwangu mimi nimeona ni muhimu”, amesema Prof. Shivji.

“Sokoine alipenda kilimo na alikuwa anaamini kuwa kijiji ni chimbuko la kuleta mapinduzi ya kijani kwa maana gani kubadilisha fikra za kuamini kwamba ukiwa mkulima wewe ni maskini alikuwa hazipendelei kwa sababu ardhi na maliasili nyingine zote zipo kijijini sasa kwa nini mkulima ajione ni maskini wakati maliasili zote zipo kijijini”, amesema Prof. Sibuga.

 



Post a Comment

0 Comments