SUAMEDIA

SUA kuendelea kutoa mafunzo kwa Viongozi ili kuleta tija chuoni

 

Na: Farida Mkongwe

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeahidi kuendelea na utaratibu wa kutoa mafunzo kwa viongozi wapya watakaokuwa wanateuliwa kutumikia nafasi mbalimbali ili kuwajengea uwezo wa namna ya kuzitumikia nafasi hizo.

Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Mipango, Fedha na Utawala (SUA) Prof. Amandus Muhairwa akizungumza na vyombo vya habari wakati wa kufunga mafunzo ya uongozi kwa Viongozi wa SUA (Picha na Mabula Musa)


Kauli hiyo imetolewa Aprili 4, 2024 mjini Morogoro na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Mipango, Fedha na Utawala Prof. Amandus Muhairwa wakati akifunga mafunzo ya uongozi kwa Viongozi wa SUA ambapo amesema hiyo ni hatua ya kwanza ya kuwawezesha viongozi hao kujitambua na kutambua hisia za wafanyakazi wenzao.

Prof. Muhairwa amesema mafunzo hayo yametolewa ili kuwatengenezea viongozi hao mazingira mazuri ya kufanyia kazi kwani wameweza kuzijua mbinu za kuongoza pamoja na kupata mafunzo ya masuala ya akili ya hisia na afya ya akili vitu ambavyo vinaathiri sana utendaji wa wafanyakazi.

“Ni utaratibu unaofanywa na Taasisi yetu kwa viongozi wapya, kama mlivyoona mafunzo yamekuwa mazuri kwa sababu kama una walimu, wafanyakazi na viongozi ambao akili zao za kihisia zina matatizo maana yake utendaji wao utaathirika lakini ukijua namna ya kufanya kazi na mtu wa namna hiyo tija itaongezeka kwenye Taasisi”, amesema Prof. Muhairwa.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Menejimenti Rasilimali Watu na Utawala SUA Peter Mwakiluma amesema wameandaa mafunzo hayo kwa sababu kwanza ni takwa la kisheria kila kiongozi mpya anapochaguliwa ni lazima apitie mafunzo ya uongozi kwa sababu mtu anaweza kuwa na uzoefu wa kufanya kazi lakini hajui kabisa uongozi na matokeo yake kunakuwa na ukiukwaji wa miongozo ya Serikali Kuu.


Mkurugenzi wa Menejimenti Rasilimali Watu na Utawala SUA Peter Mwakiluma

akizungumza na Viongozi wa SUA (hawapo pichani) kabla ya kufungwa kwa mafunzo hayo 
(Picha na Mabula Musa)

“Pili ni kuwaingiza rasmi sasa kwenye uongozi, mafunzo haya sasa ndiyo kama yalikuwa yanawasimika viongozi hawa wapya ili wajue mbali na kupata uteuzi lakini wafahamu namna gani wanapaswa kusimamia masuala yote yanayohusika na nafasi zao za uongozi, wazingatie itifaki, sheria na miongozo ya utumishi wa umma”, amesema Mwakiluma.






Post a Comment

0 Comments