SUAMEDIA

Naibu Waziri Mkuu Mhe. Doto Biteko apongeza Uhai na uimara wa SUA

 Na: Farida Mkongwe

Uhai na uimara wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) katika tafiti, utoaji wa huduma za ushauri wa  kitaalamu pamoja na huduma za ugani umechangia kwa kiasi kikubwa kuongeza uzalishaji na tija katika Sekta ya Kilimo nchini.

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Mh. Dkt. Doto Biteko akifungua Mdahalo wa kitaifa Kumbukizi ya miaka 40 ya Hayati Edward Moringe Sokoine (Picha zote na Ayoub Mwigune, Mabula Mussa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia)

Kauli hiyo imetolewa Aprili 8, 2024 na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Mh. Dkt. Doto Biteko wakati akimwakilisha Rais wa Zanzibar Mh. Hussein Mwinyi kwenye ufunguzi wa Mdahalo wa kitaifa wa Kumbukizi ya miaka 40 ya Hayati Edward Moringe Sokoine iliyofanyika mjini Morogoro.

Dkt. Biteko amewaasa Viongozi wa SUA kuendelea kutoa mafunzo ya kuzalisha wataalamu wenye ujuzi katika sekta ya kilimo na mifugo na kuifanya sekta hiyo iwe kimbilio la watu wengi hasa vijana ambao ndio nguvu kazi ya taifa.

“Mkifanya hivyo mtaendelea kumuenzi kwa vitendo yeye ambaye mmebeba jina lake kwenye Chuo chenu kwa kuwafanya vijana wa nchi hii wakaigeukia sekta ya kilimo kama chanzo cha ajira na chanzo cha kukuza uchumi wao”, amesema Dkt. Biteko.

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Mhe. Dkt. Doto Biteko aliyekaa (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wanafamilia ya Hayati Sokoine waliosimama, kushoto aliyekaa ni Makamu wa Rais na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano mstaafu na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba na kulia ni Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof. Mkenda

Akizungumzia maisha ya Hayati Sokoine, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof. Adolf Mkenda amesema Kiongozi huyo alikuwa ni mzalendo mwenye uadilifu, shujaa na asiyekuwa na mzaha katika utendaji kazi ambapo matokeo ya kazi zake yalionekana kwa vitendo sio maneno.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof. Adolf Mkenda akizungumza katika Mdahalo la Kumbukizi ya miaka 40 ya Edward Moringe Sokoine

Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Chuo cha SUA Prof. Raphael Chibunda amesema lengo la kumbukizi hiyo kukumbuka na kutoa taarifa kwa umma na kizazi kipya kuhusu mambo taifa limerithi kutoka kwa Kiongozi huyo ikiwa ni pamoja na uongozi bora, uzalendo, uadilifu, uaminifu na kufanya kazi kwa bidii.

Makamu Mkuu wa Chuo cha SUA Prof. Raphael Chibunda akitoa taarifa ya Kumbukizi ya miaka 40 ya Hayati Edward Moringe Sokoine

“Kauli Mbiu ya Kumbukizi ya miaka 40 ya Edward Sokoine ni Urithi wa Taifa katika Uongozi wake, Bidii, Uadilifu na Uamifu, hii inalenga kuwawezesha vijana kuenzi historia , urithi usiofutika na misingi imara ya uongozi iliyoachwa na Hayati Sokoine ambayo itatumika kama rejea ya kuongoza vijana na vizazi vya sasa na vijavyo”, amesema Prof. Chibunda

Picha chini ni matukio mbalimbali wakati wa Kumbukizi hiyo 👇







Post a Comment

0 Comments