SUAMEDIA

SUA kuendelea kunufaika na miradi inayofadhiliwa na nchi ya Norway

Na ; George Joseph

Balozi wa Norway nchini Tanzania Mhe. Tone Tinnes ameahidi kushirikiana na Chuo kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kwa kuendeleza miradi inayofadhiliwa na Serikali ya Norway sanjari na kubuni na kuanzisha miradi mingine inayohusu Kilimo na Mabadiliko ya tabianchi.



Balozi Tinnes ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na menejimenti ya Chuo baada ya kufanya ziara chuoni hapo yenye lengo la kupitia miradi inayofadhiliwa na Serikali ya nchi yake pamoja na kupata uelewa wa kazi zinazofanywa katika miradi hiyo ili kuweza kujua aina nyingine ya miradi inayoweza kufanyika hapa nchini kwa kushirikiana na taifa lake katika kipindi cha ubalozi wake.

Moja ya sehemu ambayo Balozi huyo ametembelea ni Kituo cha Taifa cha Kuratibu Kabon (NCMC) kilichopo SUA ambacho kilichojengwa kwa ufadhili wa Serikali ya Norway na kupokea maelezo ya namna Kituo hicho kinavyofanya kazi zake kutoka kwa Mratibu wa NCMC Prof. Eliakimu Zahabu.

Katika maelezo yake Prof. Zahabu amesema Kituo hicho kimeandaa mradi ambao utawezesha kutengeneza mfumo wa kompyuta ambayo itamuwezesha mtu yeyote duniani kuweza kufanya maombi ya kusajili mradi na kituo kikaweza kufanya usajili huo.

Mradi mwingine ambao utafanywa na Kituo hicho ni mradi wa kuwezesha kupima gesi joto kwenye sekta zote nchini ambapo kupitia mradi huo watumishi mbalimbali watajengewa uwezo wa kuitumia mifumo hiyo.

Prof. Zahabu amebainisha kuwa Miradi hiyo waliyoiandaa na kuiwasilisha kwa Balozi ni Miradi ya miaka mitano kuanzia mwaka 2024/2025 mpaka 2028/29 ambayo itagharimu takribani dola za kimarekani milioni 5 na kwamba mwaka wa kuanza kwa miradi husika unategemea upatikanaji wa fedha hizo.

Aidha Profesa Zahabu amesema kupitia miradi hiyo kituo kitaweza kufanya kazi zake kwa ufanisi na kuwafanya wanafunzi wengi zaidi kuweza kutumia kwa kujifunza.

Hii ni mara ya kwanza kwa  Balozi wa Norway hapa nchini kufanya ziara ya kutembelea Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) tangu alipoanza majukumu yake ya ubalozi mwezi Oktoba, 2023.




Post a Comment

0 Comments