Na: Calvin Gwabara – Mbeya.
Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe. Juma
Homera kwa niaba ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amepongeza kazi
nzuri ya Utafiti iliyofanywa na SUA kwa kushirikiana na NEMC na kupelekea
matokeo yake kusambazwa kwenye nchi kumi zilizo ukanda wa magharibi mwa Bahari
ya Hindi.
Mkuu wa Wilaya ya Mbeya Mhe. Beno Malisa wakati akifunga mafunzo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe. Juma Homera.
Pongezi hizo zimetolewa kwa niaba
yake na Mkuu wa Wilaya ya Mbeya Mhe. Beno Malisa wakati akifunga mafunzo ya
siku sita kwa Maafisa Waandamizi wa Masula ya Maji na mazingira kutoka kwenye
nchi nne ikiwemo Madagaska,Msumbiji,Kenya na mwenyeji Tanzania ikiwa ni sehemu
ya kusambaza matokeo ya Mradi wa Utafiti wa Usimamizi Endelevu wa Madakio ya
Maji Kupitia Tathmini ya Kuimarisha Mtiririko wa Maji kwa Mazingira na
Utekelezaji wake katika Kulinda Ukanda wa Magharibi mwa Bahari ya Hindi na
Athari za Shughuli za Kibinadamu Tanzania (EFLOWS).
“Kwa niaba ya Mkoa wa Mbeya nitumie
nafasi hii kukipongeza Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo kupitia kwa Mtafiti
Mkuu wa Mradi huu wa EFLOWS Prof. Japhet Kashaigili amabye ndiye mratibu wa
mafunzo haya kwa kazi nzuri waliyoifanya
hadi sasa ambapo tunaona matokeo yake yamewezesha nyinyi nyote kukutana nchini
Tanzania ili kuona na kujifunza matokeo mazuri kwa lengo la kwenda kuyatumia
kwenye nchi zenu ili kulinda mtiririko salama
wa maji kuelekea baharini” alifafanua Mhe.Malisa .
Amesema anaamini kuwa elimu
waliyoipata kupitia Wataalamu wabobevu kwenye masuala ya Tathimini ya maji kwa
mazingira kutoka Tanzania na Australia yatawawezesha kupata maarifa na mbinu
ambazo zitasaidia wao kutekeleza vyema mipango na kusimamia masuala ya
usimamizi wa mito na vyanzo vya maji kwa maslahi mapana na binadamu, Mazingira
na miradi mingine muhimu inayotegemea maji na ikolojia nzima.
Kwa upande wake Mtafiti Mkuu wa
Mradi huo ambaye ni Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Uzamili, Utafiti, Uhawilishaji
wa tekanolojia na Ushauri wa kitaalamu kutoka SUA Prof. Japhet Kashaigili
amesema utafiti huo ni moja kati ya Miradi mitatu inayofadhiliwa na Programu ya
WIOSAP nchini Madagaska, Tanzania na Msumbiji
katika kipindi cha miaka miwili na nusu.
“Lengo la mradi huo ilikuwa ni
kupunguza athari za shughuli za kibinadamu ili kuimarisha Mtiririko wa Maji kwa
Mazingira na Utekelezaji wake katika Kulinda Ukanda wa Magharibi mwa Bahari ya
Hindi Kupitia Tathmini ya Kuimarisha Mtiririko wa Maji kwa Mazingira na
Utekelezaji wake kwa ufadhili wa Mkataba wa Nairobi (Nairobi Convention) fedha
ambazo ni michango ya nchi wananchama ikiwemo Tanzania” alifafanua Prof.
kashaigili.
Aidha, Prof. Kashaigili amesema
mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo mameneja na Wataalamu kwenye nchi
wananchama wa Ukanda wa Magharibi mwa bahari ya Hindi kwenye masuala ya
Tathimini ya maji kwa mazingira na dhana ya “Kutoka kwenye chanzo hadi Baharini”
(Source to Sea) hasa katika kipindi hiki ambacho kuna changamoto kubwa za
uharibifu wa mazingira na vyanzo vya maji duniani.
Ameongeza kuwa mafunzo hayo pia
yatasaidia kujenga na kuzitazama mbinu shirikishi ambazo zinaweza kutumika
kusaidia kukabiliana na changamoto ya athari za mtiririko wa maji kwa mazingira
pamoja na uchafuzi wa mazingira katika bahari na athari zake kwa viumbe maji.
Nae Wakili wa Serikali Mkuu
kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Bwana Wankyo Mnono amesisitiza umuhimu wa
ushirikino kwa nchi zote zilizo Magharibi mwa ukanda wa bahari ya Hindi kwakuwa
ulinzi wake unahitaji ushirikiano kwa nchi zote ili kufikia malengo ya
mtiririko salama wa maji kuelekea baharini pamoja na usalama wa bahari na
viumbe maji wengine.
Wakili wa Serikali Mkuu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Bwana Wankyo Mnono akitoa salamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira.
“Swala la ulinzi na usalama wa
bahari ya Hindi linahitaji ushirikiano kwa kila nchi katika kutelekeza
makubaliano na kusimamia mtitiko wa maji yake yanayoingia baharini, kukiwa na
usimamizi kwenye nchi moja wakati nchi nyingine ikifanya uharibifu changamoto
hizi hazitaweza kumalizika hivyo ni matumaini yangu kuwa baada ya mafunzo haya
mmetengeneza miongozo ambayo kila mmoja anakwenda kuhakikisha kwenye nchi yake
inatekelezeka” alisisitiza Wakili Wankyo.
Pamoja na mafunzo hayo pia
washiriki wamepata nafasi ya kutembea vyanzo vya maji na kuona jitihada
zilizofanywa na mradi huo wa Utafiti wa EFLOWS na Serikali kwenye eneo la
Wanging’ombe Mkoani njombe na pia kuzungumza na viongozi na Jumuiya za watumaia
maji ikiwemo jumuiya ya MBUMTILU.
Mradi wa Utafiti wa Usimamizi
Endelevu wa Madakio ya Maji Kupitia Tathmini ya Kuimarisha Mtiririko wa Maji
kwa Mazingira na Utekelezaji wake katika Kulinda Ukanda wa Magharibi mwa Bahari
ya Hindi na Athari za Shughuli za Kibinadamu Tanzania (EFLOWS) unatekelezwa na
Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo kwa kushirikiana na Baraza la Taifa la
hifadhi ya mazingira NEMC na wad au wengine kwa ufadhili wa Sekretarieti ya
Azimio la Nairobi.
MATUKIO KATIKA PICHA
Washiriki wa mafunzo hayo kutoka nchi nne za afrika wakiwa kwenye picha ya pamoja na mgeni rasmi Mkuu wa Wilaya ya Mbeya Mhe. Beno Malisa mara baada ya kufunga mafunzo hayo.
Washiriki wa mafunzo wakiangalia chanzo cha maji kwenye wilaya ya Manging’ombe Mkoani Njombe wakiwa kwenye ziara ya mafunzo kuona kazi zilizofanywa na mradi wa EFLOWS.
Washiriki wa mafunzo wakizungumza na Jumuiya ya watumia maji ya MBUMTILU iliyopo Wilayani Wanging’ombe Mkoani Njombe kuona namna jumuiya inavyoshiriki katika uhifadhi wa vyanzo vya maji.
0 Comments