SUAMEDIA

Menejimenti ya SUA yatakiwa kutenga bajeti ya wanafunzi wenye Mahitaji Maalumu

 

Na:Tatyana Celestine, Winfrida Nicolaus

Wito umetolewa kwa Menejimenti ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA  kutambua uwepo wa wanafunzi wenye mahitaji maalumu hivyo katika mipango yao ya chuo wanayoipanga wahakikishe wanawakumbuka wanafunzi hao  kwa kutenga bajeti ili kuwarahisishia wanataaluma  kuwasaidia katika ufundishaji kwani hata ikiwa wanajua mbinu za ufundishaji bila uwezeshwaji wa miundo mbinu ni kazi bure.

                                     

Amebainisha hayo Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam Shule Kuu ya Elimu Idara  ya Saikolijia na Ukuzaji Mitaala ambaye pia ni Meneja wa Kituo kinachohudumia wanafunzi na wafanyakazi wenye mahitaji maalum Dkt. Sarah Kisanga wakati akizungumza na SUAMEDIA kwenye mafunzo ya kuwajengea uwezo Wanataaluma juu ya kuwatambua watu wenye mahitaji maalum na namna ya kuwahudumia ili kuleta usawa.

                               

Dkt. Kisanga amesema jamii inayowazunguka ina wanafunzi wenye mahitaji mbalimbali ikiwemo ulemavu lakini pia wenye magonjwa endelevu hivyo kama walimu wanatakiwa  kutambua tofauti na kujua mahitaji yao ili watambue wanatakiwa kutumia mbinu zipi katika kufundisha kwa lengo la  kuwafikia kwa urahisi.

Aidha Dkt. Sarah Kisanga amesema Mradi wa HEET unaweza kusaidia kwa kiasi kikubwa zaidi ya asilimia 75 kitu pekee kinachohitajika ni kuongeza nguvu ya ushirikiano kati ya walimu, Menejimenti na Serikali ambapo kupitia hiyo wanaweza kufikia kiwango kikubwa cha kuhakikisha elimu inafikiwa hata kwa wale wenye mahitaji na kuleta usawa.

Naye Mhadhiri Mwandamizi Idara ya Mitaala na Ufundishaji SUA Dkt. Noel Makwinyi ameiomba Menejimenti ya Chuo kuendelea  zoezi hilo la kutoa mafunzo kwasababu bado wanauhitaji wa kuelewa zaidi vitu mbalimbali kutokana na maswali mengi ambayo washiriki wamekuwa wakiyauliza kwenye mafunzo hayo ikiwemo umuhimu wa kupata kozi za lugha za alama ambazo wengi wao hawajui.

                                  

“Lugha ya alama ingeweza kutusaidia sana si tu darasani hata pale tunapowasiliana na wanafunzi wenye uhitaji wa alama hizo nje ya darasa kwa maana ya ofisini, kwenye mazoezi kwa vitendo vilevile tunapokutana nao ana kwa ana hivyo chuo kingefikiria kufanya kozi kama hizi mara kwa mara basi angalau hata mara moja kwa mwaka”, amesema Dkt. Makwinyi




















Post a Comment

0 Comments