SUAMEDIA

Serikali yaahidi kuendeleza mijadala na chambuzi zinazochochea maendeleo

 

Na: Farida Mkongwe

Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeahidi kuendelea kuweka mijadala na kukuza chambuzi na maandishi ya kitaaluna yanayochochea maendeleo hapa nchini.


Ahadi hiyo imetolewa na Waziri wa Wizara hiyo Mhe. Prof. Adolf Mkenda wakati akimkaribisha Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Mh. Dkt. Doto Biteko ili kufungua Mdahalo wa kitaifa wa Kumbukizi ya miaka 40 ya Hayati Edward Moringe Sokoine uliyofanyika katika Kampasi ya Edward Moringe iliyopo SUA mjini Morogoro.

Prof. Mkenda alitoa ahadi hiyo baada ya Profesa Mstaafu wa Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Prof. Issa Shivji kutoa mojawapo ya nukuu iliyotolewa na Hayati Sokoine inayoelezea umuhimu wa mijadala kuhusu muelekeo  wa maendeleo ya Taifa.

Prof. Mkenda amesema tayari wameshaanza kufanya hivyo kwenye machapisho ya kisayansi na tarehe 13 watatoa tuzo ya Mwalimu Nyerere ya waandishi wabunifu huku wakifikiria kukuza waandishi wa historia ya Tanzania

Akitoa mada kuhusu Sokoine: Uongozi na Maendeleo kwenye mdahalo huo Prof. Shivji amesema Hayati Sokoine alisisitiza umuhimu wa mijadala na kusema mwelekeo wa maendeleo sahihi ni ule unaotokana na mijadala na kuongeza kuwa ni jukumu la wasomi kuchochea mijadala hiyo ambayo amekuwa haisikii kwa muda sasa.

“Sokoine hakuandika kitabu au makala ya mtazamo wa maendeleo, kwa hiyo ili kupata maono yake ya maendeleo inatubidi kuchambua hotuba zake na ningependa niwaambie vijana wetu hotuba za Sokoine mkizisoma kwa makini hazikuwa za kisiasa ni hotuba zenye mantiki ambazo zitawapa nafasi ya kujifunza mambo mengi”, amesema Prof. Shivji.

 

 




 

Post a Comment

0 Comments