SUAMEDIA

Kati ya watanzania watano (5) ni mmoja (1) tu anakumbukumbu ya Hayati Sokoine

 Na: Gerald Lwomile

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema kufuatia matokeo ya Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 kuwa idadi ya watu nchini ni milioni 61, mtu mmoja (1)  kati ya watano (5) ndiyo  anaweza kuwa na kumbukumbu ya aliyoyafanya Hayati Edward Moringe Sokoine.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia katika Kumbukizi ya miaka 40 ya Hayati Sokoine (Picha zote na Gerald Lwomile)

Akizungumza na watanzania Aprili 12, 2024 katika hotuba yake aliyoitoa katika Misa ya Kumbukizi ya miaka 40 ya Hayati Edward Moringe Sokoine iliyofanyika nyumbani kwa Sokoine Monduli Juu mkoani Arusha, Rais Samia amesema hiyo ni kutokana na ukweli kuwa asilimia 81  ya watanzania wana umri chini ya miaka 40.

Amesema Hayati Sokoine ambaye alifariki April 12, 1984 alilitumikia Taifa kwa mafanikio makubwa hivyo jambo muhimu ni kuhakikisha watanzania wanajengewa uelewa kuhusu Edward Sokoine na mchango wake kwa Taifa.

Rais Samia amesema moja ya mambo ambayo Hayati Sokoine aliyasema ni pamoja na namna vyuo vinaweza kuendesha midahalo mbalimbali ya kuona namna gani Taifa linajiletea maendeleo na kuhakikisha mawazo yao yanawafikia watunga Sera, Vyama vya Siasa na watendaji wa Serikali.

Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa akiteta jambo na Rais Mstaafu Mhe. Jakaya Kikwete wakiwa Monduli Juu Arusha

Rais Samia amesema jambo hili kwa kiasi kikubwa limekuwa likifanyika kwani wanazuoni katika vyuo mbalimbali wamekuwa wakifanya mijadala ambayo imekuwa ikisaidia kuelewa na kujua mambo mbalimbali yanayoweza kulinufaisha Taifa.

Amesema pamoja na mambo mengine Hayati Sokoine alisisitiza suala la elimu inayohitajika katika maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na vijijini basi itaimarisha ustarabu ili watu wasiridhike na maisha duni waliyonayo.

Rais Samia amesema nafarijika kuona sasa Taifa linaendelea kuwa na uwezo wa kutunza kumbukumbuka za viongozi kwani miezi michache ijayo kitabu cha Hayati Edward Moringe Sokoine kitazinduliwa.

Hivi karibuni Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kilifanya  Mdahalo wa Kitaifa wa Kumbukizi ya miaka 40 ya Hayati Edward Moringe Sokoine na mgeni rasmi alikuwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Mhe. Dkt. Doto Biteko ambaye pia alipongeza mdahalo huo.



Post a Comment

0 Comments