SUAMEDIA

Ushirikiano wa SUA na Chuo Kikuu cha Artemisa cha Cuba utainua taaluma, ujuzi na kunufaisha wananchi - Dkt Bermundez

 Na: Gerald Lwomile

Imeelezwa kuwa ushirikiano ulioanzishwa kati ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) na Chuo Kikuu cha Artemisa cha Jamhuri ya Cuba utakuwa na manufaa makubwa baina ya vyuo vikuu hivyo kwani utainua taaluma, ujuzi na kunufaisha wananchi wa pande zote mbili yaani Tanzania na Cuba.

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Prof. Raphael Chibunda akimpa zawadi ya kalenda Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Artemisa Dkt. Adianez Bermundes (Picha na Ayoub Mwigune)

Akizungumza  na viongozi mbalimbali wa Manejimenti ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Januari 25, 2024. Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Artemisa Dkt. Adianez Bermundes amesema mahusiano baina ya pande hizo mbili yatawajengea uzoefu, ujuzi na taaluma wanafunzi na wanataaluma kwa kubadilishana  uzoefu, teknolojia na kufanya utafiti mbalimbali.

Ametolea mfano mazao ya mihogo, viazi na magimbi kuwa ni baadhi ya mazao ambayo yamefanyiwa na yanaendelea kufanyiwa tafiti katika Chuo Kikuu cha Artemisa ili kuona ni kwa namna gani watu wanaweza kuendelea kuyatumia huku wakichanganya na vyakula vingine ili kuondoa hali ya kutegemea kula chakula cha aina moja.

Akizungumzia namna ya kuinua hali za wakulima katika maeneo ya nchi Dkt. Bermundez amesema chuo chao kimekuwa kikitoa elimu ya moja kwa moja kwa wazalishaji wa mazao jambo ambalo limekuwa na mafanikio makubwa pamoja na kuwa nchi yao imekuwa katika vikwazo mbalimbali kwa muda mrefu lakini imejimudu kwa kuwa na chakula cha kutosha.

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Artemisa Dkt. Adianez Bermundes wa pili (kulia) akisikiliza maelezo ya namna ya kutibu wanyama katika Hospitali ya Rufaa ya Wanyama iliyopo SUA.


Katika hatua nyingi ametoa ahadi kwa SUA kuwa atakiunganisha chuo hicho na vyuo vingine vinavyotoa elimu inayolingana na ile wanayoitoa SUA ili kuleta ufanisi zaidi kwa Tanzania lakini pia kwa Cuba.

Awali akimkaribisha Dkt. Bermundez Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Prof. Raphael Chibunda amesema Januari 24, 2024 SUA na Chuo Kikuu cha Artemisa vilitia saini Hati ya Makubaliano baina ya pande hizo mbili mbele ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Mungano wa Tanzania Mhe. Philipo Mpango na Makamu wa Rais wa Cuba Mhe Salvador Veldas Mesa .

Aidha Prof. Chibunda amemshukuru Dkt. Bermundez kwa kukubali kualika ujumbe kutoka SUA kwenda nchini humo mapema mwaka huu ili kuona ni kwa namna gani pande hizi mbili zitanufaika na ushirikiano huo.

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Prof. Raphael Chibunda na Makamu  Mkuu wa Chuo Kikuu cha Artemisa Dkt. Adianez Bermundes wakitia saini Hati ya Makubaliano (Picha kwa hisani ya Ofisi ya Makamu wa Rais)


Aidha Dkt. Bermundez alipata wasaa wa kujua mambo mbalimbali yaliyopo SUA ambapo katika wasilisho lake Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaalamu Prof. Maulid Mwatawala amesema chuo kimekuwa na mafanikio makubwa tangia kuanzishwa.

Akitoa neno la shukrani kwa ujio wa Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Artemisa cha Cuba, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Mipango, Utawala na Fedha Prof. Amandus Muhairwa amesema ushirikiano baina ya Tanzania na Cuba ni wa kihistoria na anatarajia ushirikiano baina ya SUA na Artemisa utaleta matunda makubwa si kwa vyuo hivyo pekee lakini kwa wanachi wote.

Akiwa Chuoni hapo Dkt. Bermundez ametembelea maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na Hospitali ya Rufaa ya Wanyama iliyopo SUA.

Matukio mbalimbali katika picha 👇








Post a Comment

0 Comments