SUAMEDIA

SUA yaendelea kuboresha Program za Chuo hicho

 

Nal: Ayoub Mwigune

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia Kurugenzi ya Uzamili, Utafiti, Uhaulishaji wa Teknolojia na Ushauri wa Kitaalam kwa siku mbili mfululizo kimeendelea kufanya mapitio ya Programu zao za Shahada za Uzamili kwa lengo la kuziboresha ili ziwe na uwezo wa kuyafikia mahitaji ya jamii ya watanzania.




Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Uzamili, Utafiti, Uhaulishaji wa Teknolojia na Ushauri wa Kitaalam Prof. Japhet Kashaigili wakati akizungumza na SUA Media ambapo amesema wamekuwa wakifanya mapitio hayo ya Mitaala chini ya Program ya HEET ambayo imewawezesha kuangalia Mitaala yao iko kwenye hali gani kwa sasa ukilinganisha na uhalisia wa soko ili waweze kuiboresha na kufikia matakwa ya soko ambapo ni jambo la msingi katika kuleta manufaa yenye tija.

Amesema mapitio hayo yamefanywa na wataalam wa Chuo lakini pia yamewahusisha wadau mbalimbali ambao ni wanafunzi waliohitimu Chuoni hapo, wadau kutoka taasisi mbalimbali za kiserikali pamoja na za umma na watu binafsi ambao wanavutiwa na program zinazotolewa na SUA na kwamba zoezi hilo ni la msingi kwa kuwa linawawezesha kujua aina ya program walizonazo na zinahitaji nini ili kuweza kuwa na mvuto zaidi na hivyo kuweza kupata wanafunzi wengi kwenye Chuo hicho.

"Kwa hiyo hili ni zoezi muhimu sana kwa sababu linaonesha mustakabali wa Chuo kwa maana ya kwamba wanafunzi ambao watakuja chuoni kwetu lakini pia matumizi ya wale wahitimu wetu ni wapi wanaweza wakaajiriwa hivyo suala hili linaandaliwa kwa ajili ya kujenga maendeleo ya ujuzi kwenye suala zima la uandaaji wa hizi program ambazo tumekuwa tukiendelea kuzipitia”, alisema Prof. Kashaigili.

Aidha amesema licha ya kufanyia maboresho program zilizo kuwepo vile vile wanaanzisha program zingine mpya kulingana na hitaji la soko kwa sasa ikiwemo kuingiza masuala ya namna ya kutumia akili bandia (Artificial Inteligency) kwenye masuala ya uzalishaji na masuala  mtambuka ambayo yanaendana na soko la sasa.

Kwa upande wake Dkt. Zahra Majili amesema wanacholenga ni kuhakikisha Mitaala yao inaweza kuendana moja kwa moja na soko la ajira lakini pia hali halisi ya muhitimu anayetoka SUA kuweza kuwa na uwezo wa kupata kazi kwa haraka iwe kwa kuajiriwa au kujiajiri hivyo wanahitaji elimu ambayo itawafanya wadau wao ambao ni wanafunzi iweze kuchangia katika kuhamasisha ukuaji wa uchumi wa nchi.

Naye mmoja wa wanafunzi walioshiriki katika zoezi hilo Rafiki Hamza amesema kuwa  manufaa makubwa ya zoezi hilo ni kuwa Mitaala hiyo inalenga kutengeneza wahitimu watakaoenda kuuzika kwenye soko la ajira wakiwa na ujuzi ambao unahitajika kuendana na mabadiliko ya Kiteknolojia lakini pia mifumo ya kijamii.




Post a Comment

0 Comments