SUAMEDIA

Aina mpya ya mbegu za Tumbaku kutoka Brazil kusaidia TORITA kufikia lengo la tani milioni 200 ifikapo 2025

 Na: Calvin Gwabara – Tabora.

Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Tumbaku Tanzania (TTB) Bwana Stanley Nelson Mnozya kwa niaba ya Wakulima wa Tumbaku nchini amepongeza juhudi zinazofanywa na Serikali ya awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia Taaasisi ya Utafiti wa Tumbaku nchini TORITA kwa jitihada kubwa inazozifanya katika kuwezesha upatikanaji wa mbegu bora za Tumbaku ili kuongeza uzalishaji na kuinua uchumi.

 Picha ya pamoja ya Bodi ya Wakurugenzi ya Taasisi ya Utafiti wa Tumbaku Tanzania (TORITA) wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya kutembelea shamba la mbegu bora za Tuambaku kutoka Brazil.

Kauli hiyo ameitoa mara baada ya kumalizika kwa kikao cha Bodi ya Wakurugenzi wa TORITA wakati wajumbe hao walipotembelea kuona aina mpya za mbugu bora za Tumbaku zinazojaribiwa kutoka nchini Barazil ambazo zinauwezo mkubwa wa kuzalisha Tumbaku kuliko mbegu ambazo wakulima wamekuwa wakizitumia kwa miaka mingi hapa nchini.

“Tumeona haya majaribio ya mbegu mpya za Tumbaku ambayo TORITA inaendela nayo hapa Tabora, tumeona majaribio kama matano hivi ambazo ni mbegu mpya toka nchi ya Brazil hili na jambo kubwa sana ambalo linafanywa na Serikali yetu kwenye sekta ya Tumbaku, tunavyoona mbegu zinazidi kuingia aina kwa aina tena kutoka nchi zinazosifika kwa kilimo cha Tumbaku duniani inatupa moyo sana” alieleza Bwana Stanley.

Aliongeza “Kwa niaba ya Wakulima wa Tumbaku nchini niwapongeze TORITA kwa kazi hii nzuri iliyotukuka lakini ni kazi ambayo inaunga mkono jitihada za Mama yetu Dkt. Samia suluhu Hassan kupitia Waziri wake wa kilimo Mhe. Hussein Bashe ambayo amekuwa akiifanya usiku na mchana kuhakikisha sekta ya Tumbaku inatulia na wote tunaona katika miaka miwili mitatu iliyopita tulikuwa tunaongelea uzalishaji wa tani milioni 37 za Tumbaku  nchi nzima lakini mwaka huu 2022/2023 uzalishaji umeenda hadi kilo milioni 122 na zao kuingia dola za kimarekani zaidi ya milioni 286 kwa nchi nzima”.

Ametumia nafsi hiyo kuwaasa wakulima kuamka na kujiandaa kwa mabadiriko makubwa katika upatikanaji wa mbegu bora zenya tija kubwa kwakuwa Serikali hii inafanya jitihada kubwa za kuhakikisha inawakomboa na kuwainua kwakuwa mbegu hizo walizoziona zikifanyiwa majaribio zinafanya vizuri sana kuliko mbegu walizonazo wakulima kwa sasa hivyo ni neema kwa wakulima wa Tumbaku nchini.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TORITA kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) Prof. Gration Rwegasira amesema kuwa mbegu hizo zinazofanyiwa majaribio kutoka Brazil ni sehemu tu ya mahitaji ya soko lakini TORITA inazalisha aina mbalimbali za mbegu na kuboresha zile ambazo zinatumiwa na wakulima nchini kwa sasa lakini pia wanazalisha kulingana na uhitaji wa soko kama la Marekani, Asia na kwingineko.

“Tunaishukuru sana Serikali kwa namna inavyoisaidia TORITA lakini tungeomba wanapoweka ruzuku katika uzalishaji wa mbegu za mazao mbalimbali wakumbuke sana zao la Tumbaku kwakuwa halina kampuni binafsi inayoizalisha mbegu ya Tuambaku wala Taasisi kama ASA ambao wanazalisha na kusambaza mbegu za mazao mengine, Mbegu za Tuambaku zinazalishwa na TORITA tu nchini.” Alifafanua Mwenyekiti wa Bodi Prof. Rwegasira.

Hivyo ameiomba Serikali inapoitikia kwenye masuala ya mbegu iweze pia kuingalia TORITA na kuingozea fedha ili iweze kuzalisha mbegu za aiana mbalimbali na za kutosha na kuwezesha wadau waweze kuzipata mbegu hizo bora hapahapa nchini.

“Tunajua Serikali iliweka mkazo kuwa mbegu za mazao mbalimbali yanayolimwa nchini zizalishwe hapa hapa ndani na sio zitegemewe kutoka nje, jambo ambalo TORITA ililiitikia na kulifanyia kazi kwa bidii na kuhakikisha mbegu za Tumbaku zinazalishwa hapahapa nchini na tunaweza kusema sasa kuwa tuna mbegu za kila aina za kuwafaa wadau wote kulingana na mahitaji ya soko hivyo Serikali itusaidie tuzizalishe kwa wingi mbegu hizi zipatikane kwa wadau ili kufikia malengo yake ya wakulima kupata mbegu bila vikwazo” alieleza Prof. Rwegasira.

Nae Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Tumbaku (TORITA) Dkt. Jacob Bulenga Lisuma amesema kuwa kwenye jaribio hilo la mbegu kutoka Brazil zipo za aina tatu ambazo ni AOV 12, AOV 405 na AOV 815 na zinapambanishwa na Mbegu aina ya RG 17, K326 ili kuangalia uzalishaji wake.

 “Tumeshafanya majaribio kwa miaka miwili na tumeweza kuzalisha kilo 3425 kwa hekta huu ni uzalishaji mkubwa sana, sasa jaribio hili lipo katika awamu ya mwisho na tunafanya kwa kushrikiana na Taasisi ya Uthibiti wa Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI) na jaribio hili likikamilika hatua za usajili zitafuta” Alifafanua Dkt. Jacob.

Amesema pamoja na uzalishaji wa mbegu hizo kuwa mkubwa ikilinganishwa na mbegu zinazolimwa sasa na wakulima lakini sifa nyingine kubwa ni uwezo wa mbegu hizo katika kukinzana na magonjwa ya Minyoo fundo (nematode) ambao wanasababisha Tumbaku kudumaa.

Aidha amesema kutokana na ongezeko kubwa uzalishaji lililopatikana na mwaka huu kutoka tani milioni 37 za Tumbaku  nchi nzima hadi tani milioni 122 mwaka huu 2022/2023, ana imani kuwa kuanza kutumika kwa mbegu hizo mapema wanaweza kufikia lengo walilopewa na Serikali katika sekta ya Tumbaku la kuzalisha tani milioni 200 ifikapo mwaka 2025.

Mkurugenzi huyo wa TORITA amesema tayari chama kimeshamshukuru Waziri wa kilimo Mhe. Bashe kwa jitihada zake za kufikia uzalishaji huo mkubwa kwa mwaka huu na kipande kilichobaki kwenda kwenye tani milioni 200 kutoka kwenye tani 122 ni kitu kidogo sana na takwimu zitaonesha namna Tumbaku inavyoiingizia nchi fedha nyingi za kigeni.

Amesema kulingana na taratibu za usajili wa mbegu nchini mbegu hizo zinazofanyiwa majaribio zinaweza kuanza kulimwa na wakulima mwaka 2026/2027 ila kama zitawahi kwa kufuata taraibu zinaweza kuwafikia wakulima mwaka 2025/2026.

Dkt. Jacob ameshukuru mchango mkubwa unaotolewa na Bodi ya wakurugenzi ya TORITA katika kutimiza malengo ya uanzishwaji wa Taasisi hiyo na hivyo kuahidi kuendelea kusaidia lengo kubwa la Wizara ya kilimo la Sekta ya kilimo kuweza kuchangia asilimia 10 kwenye pato la Taifa ifikpo mwaka 2030.


Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Tumbaku Tanzania (TTB) Stanley Nelson Mnozya akito salamu za shukrni kwa kazi nzuri inayofanywa na TORITA katika kuinua uzalishaji wa Tumbaku nchini.



 Mwenyekiti wa Bodi ya wakurugenzi ya TORITA (wa kwanza kushoto) kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) Prof. Gration Rwegasira akitoa salamu za bodi yake.


Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Tumbaku (TORITA) Dkt. Jacob Bulenga Lisuma (wa kwanza kulia) akijibu maswali na kutoa ufafanuzi kwa wajumbe wa bodi kwenye shamba hilo la majaribio.



 Mtafiti kutoka TORITA Bi. Magdalena Ntatilwa akitoa ufafanuzi kwa wajumbe wa bodi kuhusu mbegu hizo zinazofanyiwa majaribio.


 Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Tumbaku (TORITA) Dkt. Jacob Bulenga Lisuma (wa kwanza kulia) akijibu maswali na kutoa ufafanuzi kwa wajumbe wa bodi kwenye shamba hilo la majaribio.



Post a Comment

0 Comments