SUAMEDIA

Wizara ya Kilimo kuendeleza mashirikiano na USAID kuinua Kilimo

 Na Gerald Lwomile

Wizara ya Kilimo nchini imesema itaendelea kuwa na ushirikiano na Shirika la Misaada la Kimataifa la Marekani (USAID) katika kuhakikisha inainua sekta ya kilimo nchini ambayo imekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya wakulima.

 Mratibu Wizara ya Kilimo Mashirikiano ya Kimataifa Bibi. Daines Mtei  aliyevaa kilemba katikati akipata maelezo mbalimbali kutoka kwa wadau wa kilimo

Akizungumza katika sherehe za mwaka mmoja tangu kuanza kwa Program ya Kilimo Tija inayoendeshwa kwa ufadhili wa USAID, Mratibu Wizara ya Kilimo Mashirikiano ya Kimataifa Bibi. Daines Mtei amesema Wizara imekuwa ikitaka kuhakikisha kilimo kinamnufaisha mkulima, kiwe cha ajira na kitengeneza kipato kwa mkulima ili aweze kuendesha maisha yake.

Bibi. Mtei amesema nchi imepata matokeo chanya katika kilimo kupitia misaada mbalimbali inayotolewa na USAID na kuongeza uzalishaji wa mazao ya kilimo hivyo wanaona umuhimu wa kuwepo kwa shirika hilo la misaada nchini.

Amesema ushahidi wa matokeo hayo chanya unathibitishwa na ushirikiano ulipo baina ya Chuo cha Kilimo MATI Ilonga na USAID kupitia mradi huo wa Kilimo Tija ambapo malengo kadhaa yamefikiwa ikiwa ni pamoja na kuboresha mifumo ya masoko ya mbogamboga na matunda ili kupanua wigo wa fursa za ajira na uchumi.

Amesema katika kutekeleza ushirikiano huo USAID imewezesha uwepo wa miundombinu ya umwagiliaji ikiwemo bwawa, pampu na mazao ya kuanzia huku chuo cha MATI Ilonga kikijikita katika kuunganisha miundombinu hiyo pamoja na eneo la kutekeleza mradi huo.

Mratibu Wizara ya Kilimo Mashirikiano ya Kimataifa Bibi. Daines Mtei akizungumza katika sherehe za mwaka mmoja wa Kilimo Tija

Awali akizungumza katika sherehe hizo Mkuu wa Program ya Kilimo Tija Tanzania Bw. Antonia Coello amesema katika utekelezaji wa program hiyo ndani ya mwaka mmoja kuna mafanikio kadhaa  ambayo wamepata ikiwa ni pamoja na zaidi ya asilimi 56 ya wadau waliotegemea kushiriki katika program miongoni mwao elfu saba ni vijana na asilimia 39 ni wanawake.

Mkuu wa Program ya Kilimo Tija Tanzania Bw. Antonia Coello akizungumza wakati wa sherehe hizo

Amesema program hiyo hadi sasa imewafikia wakulima wadogo na wa kati 277 huku zaidi ya shilingi bilioni 3.9 zikitumika katika kutekeleza program hiyo ya Kilimo Tija ambapo mambo kadhaa yamefanyika ikiwa ni pamoja na kutoa mitaji, vifaa  na teknolojia mbalimbali ili kuhakikisha mradi huo unafanikiwa.

Naye Naibu Mkurugenzi kutoka Ofisi ya Ukuzaji Uchumi ya Shirika la Misaada la Kimataifa la Marekani USAID Bw. Plato Hieronimus amesema utekelezaji wa program hiyo katika Chuo cha Kilimo MATI Ilongo ni moja kati ya majukumu yao waliyojiwekea ili kusaidia maendeleo katika nchi ya Tanzania.

Amesema ili wakulima wajue mbinu bora za kilimo ikiwa ni pamoja na kilimo cha umwagiliaji ni muhimu wakapata mafunzo na kujua namna bora zaidi ya kufanya kilimo na hilo litaletwa na uhusiano imara zaidi kati ya Wizara ya Kilimo, Wadau na Sekta binafsi kwani bila wao ni vigumu kuwa na muendelezo katika kilimo.

Naibu Mkurugenzi kutoka Ofisi ya Ukuzaji Uchumi ya Shirika la Misaada la Kimataifa la Marekani USAID Bw. Plato Hieronimus akipanda mche wa nyanya

Akizungumza na vyombo vya habari wakati wa sherehe hizo Mkuu wa Chuo cha Kilimo Ilonga Bw. Felix Mrisho amesema Chuo hicho kimeingia makubalianao na Mradi wa Kilimo Tija ambao ulianza tarehe 14 Aprili, 2023 lengo likiwa ni kutoa mafunzo kwa vijana.

Amesema wamefundisha vijana wengi wakiwemo wale wa BBT Pamoja na vijana wanaosoma katika chuo hicho cha MATI Ilonga na wamefundishwa mambo mbalimbali ikiwa ni Pamoja na kuchagua eneo sahihi la uzalishaji, namna ya kuandaa shamba, matumizi ya mbolea, kufunga mifumo ya umwagiliaji na matumizi bora ya maji na namna ya kupambana ili mazao yasishambuliwe na wadudu na kilimo biashara.

Mkuu wa Program ya Kilimo Tija Tanzania Bw. Antonia Coello (wa pili kulia) akibadilishana mkataba wa makubaliano na Mkuu wa Chuo MATI Ilonga Bw. Felix Mrisho akiyevaa kofia wakati wa sherehe hizo







 Matukio katika picha wakati wa sherehe hizo


Post a Comment

0 Comments