SUAMEDIA

Waziri wa Elimu Mhe. Prof. Mkenda aongoza timu ya Tanzania KWENYE Mkutano wa ACAT jijini Nairobi.

 Na: Calvin Gwabara – Nairobi.

Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Prof Adolf Mkenda ameongoza timu ya Serikali ya Tanzania kwenye mkutano mkubwa wa Teknolojia za Kilimo Afrika (ACAT) ulioanza leo jumatatu nchini Kenya.

Waziri wa Elimu Sayansi an Teknolojia Mhe. Prof. Adolf Mkenda akiambatana na Balozi wa Tanzania nchini Kenya Mhe. Dkt. Benard Kibesse na Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH Dkt. Amos Nungu wakitembelea maonesho nje ya ukumbi wa Mkutano.

Mara baada ya kufika kwenye viwanja vya mkutano huo mkubwa akiongozana na Balozi wa Tanzania nchini Kenya Mhe. Balozi Dkt. Benard Yohana Kibesse pamoja na Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) Dkt. Amos Nungu na watumishi wengine wa Serikali ametembelea maonesho mbalimbali ya Teknolojia za kilimo zinazooneshwa nje ya mkutano huo.

“Nimeona maonesho ambayo kimsingi ni kuhusu jinsi Sayansi na Teknolojia inavyoweza kuleta mabadiliko chanya kwenye kilimo pamoja na ukweli huu tumeona pia umuhimu wa kuzingatia usalama na afya kwenye mabadiliko haya na pia kuchukua tahadhari tusipoteze umiliki wa yale tunayogundua, hasa mbegu bora, ili tusiingie kwenye utegemezi utakaotudhoofisha” alisema Prof. Mkenda.

Tanzania kupitia wizara yake ya Elimu Sayansi na Teknolojia na taasisi zilizo chini yake imekuwa ikitoa mchango mkubwa katika kuhakikisha nchi inawezesha wabunifu kupitia Programu zake mbalimbali ikimwemo Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi Teknolojia na Ubunifu ( MAKISATU) ambayo yanafanyika kila mwaka kwa kuhusisha wabunifu mbalimbali kuanzia kwenye jamii, Shule za Msingi na Sekondari, Vyuo Vya kati, Vikuu pamoja na Taasisi za Utafiti na kuwapatia washindi fedha na mahitaji mengine ili kuwezesha kukuza bunifu zao na kuzibiasharisha.

Aidha Mkutano huo wa (ACAT) umeandaliwa na Serikali ya Kenya kupitia Wizara yake ya Kilimo na Maendeleo ya Ufugaji kwa kushirikiana na Taasisi ya Teknolojia za Kilimo Afrika (AATF).




Post a Comment

0 Comments