SUAMEDIA

Wakuza Mitaala SUA wahimizwa kuandaa Mitaala Mipya ya Kidigitali kwa wakati

 

Na:Asifiwe Mbembela

Waboreshaji na Wakuza Mitaala wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia Mradi wa HEET wamehimizwa kuendelea na mchakato wa kuandaa mitaala mipya ya kidigitali ili kuendana na mpango ya Chuo unaoitaka mitaala hiyo kupelekwa kwa wadau wake ifikapo Oktoba 11 mwaka huu.

Wito huo umetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Uratibu wa Uboreshaji na Ukuzaji wa Mitaala SUA Dkt. Jamal Jumanne Athuman wakati akihitimisha mfululizo wa semina za mafunzo kwa wakuza mitaala wa Kampasi ya Mizengo Pinda iliyopo Mjini Mpanda mkoani Katavi.

Dkt. Jamal amebainisha kuwa mitaala ambayo inaendelea kuboreshwa na kukuzwa na Wahadhiri wa Kampasi zote tatu (Edward Moringe, Mizengo na Solomon Mahlangu) inatakiwa ikamilike kabla ya Oktoba 10 ili kuruhusu tarehe inayofuata kupelekwa kwa wadau kwa ajili ya mapitio ya awali ya mitaala hiyo.

 ‘‘Leo tumehitimisha mafunzo hapa Kampasi ya Mizengo Pinda ambapo tulikuwa na wawezeshaji wanne kila mmoja akiwasilisha kwenye eneo lake, sasa tunaanza zoezi lenyewe ambapo wakuza mitaala wanatakiwa kuhakikisha mpaka tarehe 11 ya mwezi wa 10 hii mitaala iwe tayari kwa ajili ya kupelekwa kwa wadau ili ijadiliwe zaidi”, alisema Dkt. Jamal ambaye pia ni Amidi wa Shule Kuu ya Elimu, SUA.

Amesisitiza kuwa mitaala ambayo inaenda kuboreshwa itakuwa ni mitaala ujuzi ambayo inajikita katika kumuandaa mhitimu mwenye uwezo mkubwa kinadharia pamoja na vitendo.

Dkt. Prisila Mkenda mmoja wa wawezeshaji wa mchakato wa uboreshaji na ukuzaji mitaala hapa chuoni akijikita katika masuala ya mabadiliko ya tabia nchi amesema kupitia maboresho hayo, wakuza mitaala wanatakiwa wajumuishe masuala ya hali ya hewa ili kutoa nafasi ya jamii kujifunza na kupata uelewa kuhusu mabadiliko ya tabianchi na namna gani ya kudhibiti athari zaidi kwa kuanzia na wanafunzi.

Amesema wanaona kama kwenye mitaala mipya kutakuwa na vipengele ambavyo vitaelezea mabadiliko ya tabianchi, wanafunzi watakuwa na uelewa wa kukabiliana na hali hiyo ikiwemo majanga ya mafuriko, ukame, pia kujua namna ya kukabiliana na wadudu waharibifu ambao wanachagizwa na mabadiliko ya tabianchi.

Mwezeshaji Prof. Ernest Kira ambaye pia ni Mhadhiri Mwandamizi SUA akizungumzia kuhusu uandaaji wa mitaala mipya ya kidigitali amesema kwenye mitaala inayokuja wanakusudia  kujumuisha umahiri wa kutenda kwa nadharia na vitendo ili wahitimu waendane na mahitaji ya soko.

Kwa upande wake, Dkt. Alcardo Barakabitze ambaye ni Mhadhiri wa SUA na mwezeshaji amewaambia washiriki wa mafunzo hayo Kampasi ya Mizengo kuwa, Chuo kinaendelea kujipanga na mabadiliko ya mitaala kwani kinakusudia kuongeza ufanisi na upatikanaji wa intaneti ili wanafunzi na waalimu waweze kuimudu mitaala mipya ya kidigitali.

Evaristus Aloyce, mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo akiongea baada ya mafunzo amesema maboresho ya mitaala ambayo wamepewa ujuzi ni muhimu kwani yataboresha  maeneo ambayo walikuwa wanayafanyia  kazi katika mitaala ya nyuma.

Post a Comment

0 Comments