SUAMEDIA

SUA kuwajengea uwezo Wahadhiri kuhusu utungaji Mitaala Mtandao

 

Na: Winfrida Nicolaus

Katika kuboresha ufundishaji unaoendana na maendeleo ya Sayansi na Teknolojia, Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo kupitia Mradi wa HEET kimeanza kutoa mafunzo kwa Wakuza Mitaala wa Chuo hicho ili kuwajengea uwezo wa uandaaji wa mitaala ya kisasa itakayoendana na wakati uliopo.




Akizungumzia mafunzo hayo, Mwenyekiti wa Kamati ya Uratibu wa Uboreshaji na Ukuzaji wa Mitaala SUA Dkt. Jamal Jumanne amesema chini ya Mradi wa HEET unaotekelezwa hapa Chuoni wanakusudia kuwa na Mitaala ambayo itakuwa na uwezo wa kuboresha ufundishaji na ujifunzaji kwa wanafunzi ikiwemo kutumia njia ya mtandao na njia ya mchanganyiko (blended).

Dkt. Jamal ameeleza kuwa kupitia mitaala ambayo inaundwa, Chuo kitakuwa na uwezo wa kudahili idadi kubwa ya wanafunzi ambao watakuwa na uwezo wa kujifunza katika njia rahisi ambayo itamruhusu kusoma akiwepo sehemu yoyote mbali na kukaa darasani.

“Hivyo leo tumeanza mfululizo wa Mikutano kwa ajili ya kuwajengea uwezo Wakuza Mitaala (Curriculum Developers) wa Chuo chetu kutoka kila Idara ambapo tumeanza na Idara zilizopo chini ya Ndaki ya Kilimo Chuoni hapa na baadaye tutaenda kwa Shule Kuu ya Uhandisi na Teknolojia na tutamalizia kwenye Kampasi yetu ya Mizengo Pinda”, alisema Dkt. Jamal Jumanne ambaye pia ni Mhadhiri Chuoni hapo.

Mwezeshaji wa mafunzo hayo kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dkt. Salome Maro amesema madhumuni ya mafunzo hayo ni kuhakikisha kunakuwa na vipengele sahihi hasa katika kutoa mafunzo kwa njia ya mtandao hivyo ni matumaini kuwa mafunzo hayo yatawaandaa vyema wakuza mitaala kuwa na ujuzi katika kuandaa programu zenye tija ili kukisaidia Chuo kuwa na uwezo wa kuandaa Wahitimu wenye sifa na mahitaji ya sasa.

Mmoja wa washiriki wa mkutano huo, Dkt. Gudila Anseli kutoka Idara ya Chakula, Lishe na Sayansi ya Mlaji SUA amesema Mafunzo ambayo wameyapata yatawasaidia kuongeza ujuzi wa kuandaa mitaala mizuri ambayo itawasaidia Wanafunzi wengi zaidi kujiunga na SUA kwani mifumo hiyo itakuwa na uwezo wa kumfundisha mwanafunzi hata akiwa eneo lolote.

Maboresho ya mitaala ikiwa ni sehemu ya mahitaji ya muhimu katika utekelezaji wa Mradi wa HEET, pindi yakikamilika yanaelezwa kuwa yatachagiza ongezeko la udahili kwa Wanafunzi wa ngazi mbalimbali Chuoni hapo pamoja na kuongeza ufanisi katika ufundishaji na ujifunzaji.






Post a Comment

0 Comments