SUAMEDIA

Wadau wa Sukari Kilombero waanza kuona matunda ya Jukwaa lao

 

Na; Gerald Lwomile - Kilombero

Wakati Tanzania ikiwa katika mkakati wa kuhakikisha inajitosheleza kwa sukari nchini ifikapo mwaka 2025 na kupunguza uagizaji wa sukari nchini ambao hugharimu zaidi ya shilingi bilioni 161 kwa mwaka wadau wa Sukari katika Bonde la Mto Kilombero wamekutana ili kupitia mpango kazi walioweka kuhakikisha wanawasaidia wakulima wa miwa kuzalisha kwa tija.

Meneja wa SAGCOT Kongani ya Kilombero Bw. John Banga aliyesimama akizungumza na wadau wa Sukari (Picha zote na Gerald Lwomile)

Miongoni mwa wadau hao ni Kiwanda cha Sukari cha Kilombero ambacho kimekusudia kuhakikisha kinapanua kiwanda hicho kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 565 ambapo ujenzi huo ulianza tangu Juni 2022.

Akizungumza katika kikao cha wadau hao Mkuu wa Idara ya Kilimo wa Kiwanda cha Sukari Kilombero Bw. Pierre Redinger amesema katika kuhakikisha uzalishaji wa miwa unafanyika kwa tija wanawaelimisha wakulima kuona kuwa wao si wafanyabiashara wa miwa tu ila ni wakulima wafanyabiashara ambao wameingia ubia na kiwanda hicho.

Mkuu wa Idara ya Kilimo wa Kiwanda cha Sukari Kilombero Bw. Pierre Redinger akizungumza katika kikao hicho

Amesema kiwanda kimekuwa na kusudi la kimkakati la kilimo na uzalishaji wa miwa wa ushindani na wa gharama nafuu, salama na endelevu ili kiwanda kiwe na uwezo wa kusaga na kutumia fursa za ukuaji wa soko la ndani hivyo kuwezesha mapato ya wakulima kutoka shilingi bilioni 75 na kufikia shilingi bilioni 165 kwa mwaka.

“ Tuna mpamgo wa kuleta teknolojia bora za kilimo cha miwa ambapo tutatumia zaidi ya shilingi bilioni 565 na ujenzi huu umeanza Juni 2022 na unatarajiwa kukamilika Julai 2024”, amesema Pierre.

Akizungumza katika kikao hicho Meneja wa SAGCOT Kongani ya Kilombero Bw. John Banga amesema Jukwaa hilo liliandaliwa na ofisi ya SAGCOT mwaka 2022 ili kuhakikisha kunakuwa na ustawi katika uzalishaji wa miwa na kushirikisha Kiwanda cha Sukari, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Wizara ya Kilimo na Wakulima limeanza kutoa matokeo chanya kwani wakulima wamefikia malengo makubwa tofauti na awali.

Meneja wa SAGCOT Kongani ya Kilombero Bw. John Banga akisisitiza jambo katika kikao hicho

“ Kwa mfano kutoka kwenye kilimo holela cha kulima kilimo cha miwa na kuingia kwenye mfumo rasmi ambao unaitwa kulima kwa mpango wa kanda yaani ‘Zone’ ambao umeleta mafanikio makubwa ambapo pia umesimamiwa na ofisi ya Mrajis wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Morogoro kwa kushirikiana na SAGCOT na kampuni ya Sukari ya Kilombero” amesema Banga,

 Naye Mwenyekiti wa Ushirika wa Kilimo na Masoko (AMCOS) wa wakulima wa miwa katika bonde la Kilombero Bw. Bakari Mkangamo amesema awali wakati kiwanda hicho kinamilikiwa na kuendeshwa na Serikali miwa ilikuwa inalimwa lakini si kwa asilimia kubwa kama ilivyo sasa kwani katika kipindi hicho wakulima wengi waliona mpunga una faida zaidi kuliko miwa kwani bei ilikuwa ndogo na wakati mwingine miwa haivunwi na kununuliwa kwa wakati jambo lililosababisha migogoro mingi.

Amesema baada ya kuja wawekezaji kwenye miaka ya 2000 tani moja ya miwa ilitoka kwenye bei kandamizi ya sh. elfu 20 kwa tani moja hadi kufikia sh. elfu 65 ambapo hivi sasa tani imefikia sh. elfu 90 jambo ambalo limehamasisha kilimo cha miwa.

Amesema mabadiliko ya uanzishwaji wa Ushirika kutoka ule wa Chama cha Wakulima wa Miwa katika bonde hilo umekuwa na manufaa makubwa kwani sheria iliyoanzishwa ya kuwalazimisha wakulima wa miwa kuwa wanaushirika imetatua mizozo mingi ikiwa ni pamoja na kuwepo kwa mpagilio mzuri wa uvunaji hata kama baadhi ya miwa itabaki shambani kwa mwaka au zaidi.

Picha chini ni wadau wa Sukari katika Bonde la Mto Kilombero








Post a Comment

0 Comments