SUAMEDIA

Mawasiliano ya tafiti yanasaidia kutatua changamoto ya mabadiliko ya tabia nchi

 Na; Hadija Zahoro

Mawasilisho ya tafiti mbalimbali kutoka nchi za nje pamoja na tafiti  kutoka taasisi za ndani ya nchi ikiwemo  SUA, zimesaidia kuonesha njia mbadala za kutatua changamoto ya mabadiliko ya tabianchi ikiwemo kurudisha uoto wa asili kwa kutumia sayansi za wananchi, sayansi ya kitaalamu ya utambuzi wa miti ya asili pamoja na mimea ya uoto wa asili kwenye vyanzo vya maji zitakazosaidia kuboresha mazingira bora kwa maendeleo endelevu nchini.

Washiriki wa Kongamano la siku mbili kwenye wiki ya Kumbukizi ya 18 ya Sokoine wakiwa katika picha ya pamoja

Hayo ameyasema Prof. Japhet Kashaigili, Mratibu wa utafiti na machapisho katika Kurugenzi ya Uzamili,Utafiti, Uhaulishaji wa Teknolojia na  Ushauri wa Kitaalamu wakati akizungumza na waandishi wa habari  Mei 24, 2023  katika Kongamano la siku mbili kwenye wiki ya Kumbukizi ya 18 ya Sokoine iliyolenga kuzungumzia suala la mazingira wezeshi kwa ajili ya kilimo.

Prof. Kashaigili amesema tafiti zilizowasilishwa katika Kongamano hilo   zimeonesha kuwa shughuli za binadamu ikiwemo kukata miti, kilimo kisicho rafiki na mazingira pamoja na ufugaji holela  ni viashiria vikubwa vinavyopelekea changamoto ya mabadiliko  ya tabianchi  na kukwamisha maendeleo endelevu nchini.

Ameeleza kuwa uoto wa asili unapotolewa inaruhusu kusambaa kwa hewa ya ukaa inayopelekea kuharibu tabaka la anga na baadae kuongezeka kwa joto duniani hivyo, ikitumika njia ya kurudisha uoto wa asili kwenye vyanzo,  inaweza kusaidia kuongeza uwezo wa maji kuvivia chini ya udongo  na kupunguza uzalishaji wa udongo unaotiririka kwenye mito  na kusababisha athari  kwenye ikolojia ya mito na mabwawa.

“Nikichukulia  mfano wa  bwawa la Mtera, Kidatu pia nikichukulia mfano jitihada kubwa ya nchi kwenye Mradi wa Mkakati wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere, utaona kwamba kama hatuwezi kupunguza kwa kutumia njia hizi mbadala za kupunguza uzalishaji wa udongo inawezekana tukaathiri maisha ya bwawa baada ya kujaa tope”,  ameeleza Prof. Kashaigili.

“Matokeo ya tafiti yametuonesha kuwa  tukiweza kufanya vizuri kwenye urudishaji wa uoto wa asili  tunaweza tukapunguza uzalishaji wa tope  ambalo linaenda kwenye mabwawa na kuongezea uwezo wa maji kuvivia kwenye udongo ambayo ni faida wakati wa kiangazi katika maana ya kuongezea uwepo wa maji wakati wa kiangazi”, ameongeza Prof. Kashaigili.

Kwa upande wake Mhadhiri Msaidizi  katika Idara ya Mimea na Vipando na Mazao ya bustani, Bi.Caroline Maro, ameeleza kuwa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo  kinawapatia wanataaluma wake fedha kwa  ajili ya kufanya tafiti mbalimbali ambazo baadae zinakuja  kutoa majibu au suluhisho ya changamoto zinazoikabili nchi hasa kutokana na madaliko ya tabia nchi.

Amesema kuwa yeye ni mmoja wa Mwanataaluma aliyenufaika na fedha zilizotolewa katika miradi  na anafanya utafiti wa kuangalia ni jinsi gani wanaweza kuboresha vyakula au kuongeza vyakula vyenye virutubisho vinavyoweza kuepukana na matatizo ya afya hasa upungufu wa madini na vitamini katika Mikoa ya Nyanja za Juu Kusini.

Kongamano hilo limejadili mada mbalimbali zilizowasilishwa na wataalam na tafiti mbalimbali zilizofanyika nchini na mawasilisho kutoka Taasisi tofauti za Serikali kama vile SUA, UDOM, Wizara ya Maji, Chuo Kikuu cha Dar es salaam na TARI pamoja na mawasilisho kutoka   nchi mbalimbali za nje ikiwemo Ethiopia na Chuo Kikuu cha Uingereza





Post a Comment

0 Comments