SUAMEDIA

Hali ya vyanzo vingi vya Mito nchini si vya Kuridhisha : Prof. Kashaigili.

 Na: Adam Maruma – Morogoro.

Imeelezwa kuwa Hali ya vyanzo vingi vya mito hapa nchini si ya kuridhisha kutokana na shughuli mbalimbali za kibinadamu zinazoendelea katika vyanzo hivyo  huku baadhi ya vyanzo  vikiwa katika hali nzuri na endelevu.

Mratibu wa Utafiti na Machapisho  kutoka Chuo Kikuu Cha Sokoine Cha Kilimo (SUA) Prof. Japhet Kashaigili ( Aliyevaa kofia) akiwa kwenye moja ya vitalu miche rafiki na maji vilivyoanzishwa na Mradi wake wa EFLOWS Mkoani Njombe kwa lengo la kurudisha uoto wa asili kwenye mito na vyanzo vya maji vya mto Mbarali. 


Hayo yameelezwa na Prof. Japhet Kashaigili ambae ni Mratibu wa Utafiti na Machapisho  kutoka Chuo Kikuu Cha Sokoine Cha Kilimo SUA wakati akizungumzia Maadhimisho  ya Siku ya Mazingira Duniani ambayo huadhimishwa na Umoja wa Mataifa kupitia shirika lake la Mazingira UNEP  kila ifikapo June 5 ya kila mwaka.

Prof. Kashaigili amezitaja shughuli zinazoharibu vyanzo hivyo ni pamoja na Ukataji miti, shughuli za Kilimo, Ufugaji, Uchomaji mkaa na Uanzishwaji wa makazi ya watu kiholela kuwa tishio kubwa la vyanzo hivyo.

 ‘’Hali ya vyanzo vingi vya mito mingi si vya kuridhisha huku baadhi ya vyanzo hivyo ikiwa ni nzuri na endelevu na hii inategemea  maeneo vyanzo hivyo vilipo na watu wanaozunguka vyanzo hivyo ni watu wa aina gani na wanafanya shughuli gani, mito mingi  ukiangalia inaanzia milimani   na  ndiko kuna shughuli za kibinadamu  huko, kwa kuwa mvua zinanyesha zaidi ukilinganisha na maeneo mengine’’, amesema Prof. Kashaigili.

Mtaalam huyo wa masuala ya Mazingira ameongeza kuwa amekuwa akifanya tafiti nyingi kwenye eneo la maji na mazingira kwa muda wa zaidi ya miaka 20 na kusema  kuwa ukataji miti na hasa miti ya asili ambayo  huondoa uoto wa asili ambao huhifadhi mito kwa kuifunika mito hiyo ili kuendeleza uasili wake na hivyo ukataji huo wa miti ya asili na mimea mingine imekua na athari kubwa kwa vyanzo vingi vya mito pamoja na vyanzo vingine vya maji.

Aidha Prof. Kashaigili amezitaja athari nyingine za shughuli za kibinadamu kwenye vyanzo vya mito au kando ya mito hiyo kuwa ni pamoja na kubadilika kwa mwenendo wa maji ya mito kwa kutawanyika ovyo na kuacha njia yake asili ambayo hupelekea kiasi cha maji na misimu ya maji kupungua kwa kiasi kikubwa kutokana na kuongezeka kwa tope katika njia ya mito hiyo.

‘’Nimekuwa nikifanya tafiti nyingi kwa zaidi ya  miaka 20 kwenye eneo la maji na athari zingine zinasabishwa kwa kiasi kikubwa na aina ya kilimo  kama  kilimo cha vinyungu, kinachofanyika kwenye vyanzo vya mito au pembeni mwa mto pamoja na shughuli nyingine zinazohusisha ukataji miti, hasa miti ya asili ambayo huhifadhi mto kwa kuifunika ili kuendeleza uasili wake sasa ukatiji wa miti hiyo ni kama kuifunua mito hiyo na kuiweka wazi na hii  inasababisha maji mengi kupotea na pia kupelekea mto kupoteza mwelekeo wa asili wa maji na kupelekea kiasi na misimu ya maji kupungua kwa kiasi kikubwa’’, Prof. Kashaigili.

Mtafiti huyo nguli wa masuala ya mazingira na maji  ameongeza kuwa uwezo na  uhifadhi wa maji kwenye mito wakati wa kiangazi inategemea aina ya uoto uliopo katika maeneo yanayozunguka vyanzo vya mito na kusema kuwa kama eneo hilo lina kiasi kikubwa cha miti iliyokatwa inayopelekea uwezo wa kuhifadhi na kunywea kwa maji kwenye udongo kwa haraka,   kwa sababu dakio la maji linakua halina uwezo wa kuhifadhi maji kwa muda mrefu kutokana na athari za shughuli zinazofanyika katika maeneo yaliyo karibu na mto huo na maji kuwa machache kipindi cha kiangazi na wakati mwingine kuisha kabisa.

Amezitaja baadhi ya maeneo yenye uhifadhi mzuri wa vyanzo vya mito kuwa ni mto Zigi uliopo katika bonde la mto Pangani mkoani Tanga, bonde la Mbarali liliopo mkoani Mbeya ambapo bonde la mto Mbarali amelitaja kama eneo ambalo bado uhifadhi wake si wa kuridhisha ukilinganisha na viwango vinavyokubalika lakini jitihada zinazofanyika na mwamko zinaonesha mwanga katika siku zijazo.

Prof. huyo ameitaka jamii kuchukulia suala la utunzaji wa mazingira kuwa la kila mmoja kwa kuzifanya shughuli zao za kila siku ziwe rafiki kwa mazingira kwani mazingira yakitunzwa vizuri na yenyewe yataitunza jamii na pia ameshauri kubuniwa kwa shughuli mbadala kama ufugaji nyuki, uanzishwaji wa bustani na kilim0 cha miti ya matunda kama mbadala wa shughuli zinzopelekea uharibifu wa mazingira.

 

 

 

Post a Comment

0 Comments