SUAMEDIA

Wahitimu katika Mahafali ya katikati ya mwaka kwa masomo SUA waongezeka

 Na: Winfrida Nicolaus

Idadi ya Wahitimu katika Mahafali ya katikati ya mwaka kwa masomo (Mid-year Graduation) katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) imeongezeka kutoka Wahitimu 209 kwa mwaka 2022 hadi 274 kwa mwaka 2023 ambapo kati ya hao watunukiwa wanawake ni 91 sawa na asilimia 33.2 ya wahitimu wote.

Makamu wa Mkuu wa Chuo Prof. Raphael Chibunda akizungumza katika mahafali ya katikati ya mwaka wa masomo

Amebainisha hayo Makamu wa Mkuu wa Chuo Prof. Raphael Chibunda wakati akitaja takwimu za Wahitimu katika Mahafali hayo yaliyofanyika katika viwanja vya Michezo vya Kampasi Kuu ya Edward Moringe ambayo yamehudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Mkuu wa Chuo hicho Jaji Mstaafu Joseph Sinde Warioba ambapo amesema katika Mahafali hayo ya katikati ya mwaka zipo jumla ya Program 56 za masomo zenye jumla ya Wahitimu 274 wakiwemo wanaume 183 na wanawake 91.

Katika takwimu hizo wahitimu 189, ni kutoka Shahada za Kwanza ambapo wanaume ni 131, na wanawake 58, Shahada za Umahiri wahitimu 48 wanaume 24, na wanawake 24, Stashahada ya Juu ya Elimu wahitimu 2 wote wakiwa ni wanaume, Shahada za Uzamivu 15, wanaume 10 na mwanamke 5, wahitimu wa Stashahada 18 wanaume 14 na wanawake 4 vilevile wahitimu 2 wa Astashahada wote wakiwa ni wanaume. 

Aidha, Prof. Chibunda amesema kuwa wanastahili kujipongeza kwa mafanikio ambayo wameendelea kuyapata kila mwaka ya kuongeza idadi ya nguvu kazi na yenye Taaluma stahiki katika nchi ya Tanzania ambapo mafanikio hayo yanatokana na ufanyaji kazi mzuri wa Viongozi wa Chuo, Wahadhiri na wafanyakazi wote wa Chuo hicho ambao wamewezesha kupiga hatua zaidi mwaka hadi mwaka.

Mkuu wa Chuo hicho Jaji Mstaafu Joseph Sinde Warioba (aliyekaa katika kiti kikubwa katikati) akiwa katika zoezi la kutunuku shahada mbalimbali katika mahafali

Vilevile ametoa pongezi maalum kwa wahitimu wote ambao wametunikiwa Shahada zao katika Mahafali hayo na kusema kuwa yote hiyo ni kutokana na nidhamu na bidii zao ambazo ndio siri za mafanikio katika kutafuta Elimu, hivyo amewaasa kuendelea kuwa na bidii, uaminifu na moyo wa kujituma waliokuwa nao wakati wa masomo kuendelea nao sehemu zao za kazi ili waweze kufanikiwa zaidi kukitangaza chuo vizuri.

‘‘Mahafali ni tukio la kipekee sana kokote pale duniani, kwa wahitimu tukio hili ni muda mahususi kwa kusheherekea na kutathmini miaka kadhaa waliotumia katika kuhakikisha wanafikia malengo yao aidha baadhi ya Mahafali ni muda kwa wahitimu kutafakari kuingia katika ulimwengu wa Ajira na ujenzi wa Taifa”, ameeleza Prof. Chibunda.

Ameongeza kuwa Chuo kimeendelea kutekeleza malengo na majukumu yake kupitia katika Ndaki zake zote saba (7), Shule Kuu ya Elimu, Kurugenzi na Taasisi zake tangu Mahafali ya 40 Novemba 2022 ikiwemo utekelezaji wa shughuli za mafunzo ambazo zimeendelea kufanyika chuoni hapo kama ilivyopangwa katika Kampasi zote tatu kwa maana ya Edward Moringe, Solomon Mahlangu pamoja na Kampasi ya Katavi.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) Jaji Mstaafu Mohamed Chande Othman, amesema takribani miezi sita tangu kufanyika kwa Mahafali ya 40 katika kipindi hicho Baraza limetekeleza majukumu yake makuu kwa ufanisi mkubwa ikiwemo kusimamia Menejimenti ya Chuo ili itimize majukumu ya chuo ambayo ni kutoa Mafunzo, kufanya Tafiti, kutoa Huduma za Kitaalam na Ugani vilevile kuzalisha Mali.

Pichani chini ni matukio mbalimbali katika mahafali 






Post a Comment

0 Comments