SUAMEDIA

Bei elekezi ujenzi wa barabara kuimarisha miundombinu hiyo nchini

 Na; Gerald Lwomile

Kufuatia kuwepo kwa gharama holela za ujenzi wa barabara nchini, Serikali kupitia Baraza la Taifa la Ujenzi (NCC) imeamua kuandaa miongozo ya msingi itakaohakikisha inakidhi bajeti ya taifa inayoandaliwa kwa mwaka na kuhakikisha barabara zinazojengwa au kukarabatiwa zinakuwa na ubora unaostahiki.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Baraza la Taifa la Ujenzi Mhandisi Dkt. Matiku Mturi akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani)

Hayo yamesemwa Juni 20, 2023 na Afisa Mtendaji Mkuu wa Baraza la Taifa la Ujenzi Mhandisi Dkt. Matiku Mturi, wakati akiongea na waandishi wa habari mjini Morogoro kwenye kikao kazi cha wadau wa barabara.

“Kila Serikali inapotaka kujenga mradi wowote inakuwa na bajeti, yale makisio ya bajeti kwa kiasi kikubwa yanatokana na gharama za ujenzi wa kilometa moja ya barabara ‘unit cost’ na ile kilometa moja inajengwa kwa kiasi gani inapatikana kwa kuwa na gharama za ujenzi au ukarabati wa kazi moja moja ambazo zinapelekea kujenga hiyo kilometa moja ‘unit rates’ kwa hiyo hii ni kazi ya msingi kujua gharama za ujenzi” amesema Dkt. Mturi

Amesema pamoja na kufanya kazi hiyo ya kutengeneza muongozo wa gharama lakini wanatambua kuwa barabara hizo zinaweza kutofautia kwani zipo ambazo zinaweza kubeba magari makubwa yenye uzito mkubwa na zile za kawaida kulingana na matumzi ya barabara husika.


Dkt. Matiku amesema mara baada ya kazi hiyo kukamilika wanatarajia kuona makandarasi wanapata ushindani wa kihalali kwani kuna wakati wakandarasi wasio na viwango huweka bei ndogo ili kuwapa zabuni na matokeo yake kazi inafanyika chini ya viwango

Naye Afisa Ujenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Ujenzi Mhandisi Tumaini Lemunge amesema sasa hivi kumekuwa na mkanganyiko wa bei kwa wakandarasi na kila mkandarasi amekuwa akija na bei yake ya ujenzi wa barabara kwa kilomita moja ili ashinde zabuni.

Afisa Ujenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Ujenzi Mhandisi Tumaini Lemunge akifafanua jambo kwa waandishi wa habari

Amesema kutokana na bei hiyo elekezi itakayopatika itakuwa ni rahisi kupata wakandarasi wenye viwango na watakaofanyakazi kwa kufuata taratibu ikiwa ni pamoja na ujenzi bora wa barabara

Naye Mhandisi Perpetua Kisamba kutoka Wakala ya Barabara (TANROADS) amesema hatua hiyo iliyochukuliwa na Baraza la Ujenzi la Taifa itawarahishia kazi kwa kupata wakandarasi wenye viwango, tofauti na awali ambapo Mkandarasi mwenye bei ndogo ndiye alipewa nafasi ya kujenga barabara huku baadhi yao wakishindwa kuwa na viwango bora vya kazi au kushindwa kumaliza ujenzi kwa wakati.

Mhandisi Perpetua Kisamba kutoka Wakala ya Barabara (TANROADS)

Kikao kazi hicho kimeshirikisha Wizara ya Ujenzi, Fedha, Tamisemi, Wakala ya Barabara, TRC, TARURA na Wakandarasi.

Pichani chini Wadau wa barabara wakijadili mambo mbalimbali katika kikao kazi










Post a Comment

0 Comments