SUAMEDIA

SUA kupitia Maktaba ya Taifa ya Kilimo ya Sokoine kuanzisha Kitabu kiitwacho "Kilimo cha Kisasa Mkononi Mwako (Mboga App)"

 Na: HADIJA ZAHORO

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia Maktaba ya Taifa ya  Kilimo iliyopo chuoni hapo kimeanzisha kitabu  chenye jina la Kilimo cha Kisasa Mkononi Mwako (Mboga App), chenye lengo la kuwafundisha vijana mbinu mbalimbali za uzalishaji wa mbogamboga ili kujiajiri kupitia Sekta ya Kilimo.



Akizungumza kupitia kipindi cha Kapu la Leo kinachorushwa na SUA FM, Afisa Maktaba  Bw.  Shabani Omary Chika amesema  kitabu hicho ni moja kati ya hazina  walizoaamua kuonesha  kwa vijana ambazo zinaweza kuwa muarobaini wa vyanzo vidogovidogo vya mapato.

Ameeleza kuwa  ndani ya hazina hiyo kuna maarifa  yaliyojificha yanayoweza yakamfumbua macho kijana  na kumtoa kutoka hatua moja kwenda nyingine 

Aidha, Bw. Chika amesema kuwa  vijana wamekuwa wakilalamika kuhusu ugumu wa maisha lakini kupitia kitabu hicho anaweza kujifunza jinsi ya kuotesha mbogamboga  akiwa nyumbani hata kama ni katika eneo finyu. 

Amesema licha ya kitabu hicho kuwa na nakala ngumu pia kinapatikana katika simu janja kwa kuipakua ambayo imeeleza  mbinu zote za upandaji wa mbogamboga ikiwemo namna ya  kulima, kuandaa kitalu, mazingira ya kuandaa kitalu, namna ya kumwagilia pamoja na namna ya kuotesha mbegu.

‘‘Hichi kitabu pamoja na kuwa tu kipo kwa nakala ngumu lakini pia kuna aplikesheni ambayo vijana wengi  wamekuwa na simu janja angeweza tu kuingia  katika simu janja yake  akaenda kwenye "play store"  akaandika  tu Mboga App,  akakutana na app hii na ikampa mazingira yote namna ambavyo anaweza kulima, namna anaweza akaandaa kitalu namna ya kuotesha kitalu na vitu vyote vimeelezwa katika app hii’’. Anaeleza Bw. Chika

Kwa upande wake Bi. Editha Njeu  ambaye pia ni Afisa wa Maktaba ya Taifa ya Sokoine ya Kilimo, ameeleza kuwa kitabu hicho kimeonesha  mambo mbalimbali  ikiwemo kujua uchaguzi wa eneo lenye uwezo kumudu upatikani wa mbolea, maji pamoja na wateja ili kuepuka gharama.

Amesema kitabu hicho kilichoandikwa na  Mkufunzi kutoka chuoni hapo Teophilda J. Maginga kimeelekeza pia sio lazima kununua madawa ya madukani  badala yake unaweza ukatumia dawa za asili kama vile  kupanda miti au majani mbalimbali yanayoweza kufukuza wadudu ili kuepuka kuingia gharama kwa vijana wasio na mtaji.






Post a Comment

0 Comments