SUAMEDIA

SUA kukabiliana na Changamoto za Uhaba wa Malisho, Uharibifu wa Mazingira na Ukosefu wa Ajira Tanzania Bara na visiwani Zanzibar

 

Na Editha Mloli

Wataalamu kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) wameendelea kufanya juhudi za kutatua changamoto za uhaba wa malisho, uharibifu wa mazingira na ukosefu wa ajira kwa wanawake na vijana na wameanza utekelezaji  wa mradi wa Tekinolojia ya Juncao kwa kuanza kuzalisha na kusambaza   mbegu za nyasi aina Juncao Tanzania Bara na visiwani Zanzibar.

Teknolojia hii inahusisha matumizi ya nyasi aina ya JUNCAO katika uzalishaji wa uyoga, kuhifadhi ardhi, kuzuia mmomonyoko wa udongo, pamoja na malisho kwa ajili ya mifugo ambapo asili yake ni kutoka Chuo Kikuu cha Kilimo na Misitu (FAFU) kilichoko Jimboni Fujian, nchini China.

Akizungumza na SUA MEDIA Mtaalamu wa teknolojia ya JUNCAO kutoka Idara ya Sayansi za Elimu ya Viumbehai (Biosciences), Ndaki ya Sayansi Asilia na Tumizi ya SUA, Dkt. Elly Ligate, amesema kwa kushirikiana na watafiti na maafisa kilimo visiwani Zanzibar wameanzisha vitalu vya nyasi hizo katika mashamba ya majaribio yaliyoko katika kituo cha utafiti wa mifugo kilichopo Kizimbani Unguja na Chamanangwe kisiwani Pemba.

Ameendelea kwa kusema kuwa kwa upande wa Tanzania bara wataalamu kutoka SUA wameshirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi kufanya majaribio ya uzalishaji wa nyasi hizo katika wilaya zipatazo 11 kwenye mikoa tofauti na Mbegu za Nyasi za Juncao zimeshasambazwa kwa wakulima katika wilaya za Geita, Kilindi, Handeni, Kibaha, Kigamboni, Bumbuli, Chalinze, Kilosa, Bahi, Mbarali, Dodoma pamoja na Ubungo na Kinondoni.   

Dkt. Ligate amefafanua kwamba  vituo hivi vitatumika katika kuzalisha mbegu za kutosha ili ziweze kusambazwa kwa wakulima na wafugaji nchini Tanzania ambapo Matarajio yao makubwa ni kuwafikia wafugaji wengi katika visiwa vya Zanzibar na Bara kwa kuwa mahitaji ya malisho ni makubwa katika kuelekea kuimarisha sekta ya mifugo nchini.

“Juhudi  za kutekeleza Tekinolojia ya Juncao nchini zilianza  mwanzoni mwa mwaka 2021 na zimeendelea kuenea nchi nzima na Kila tuliko peleka mbegu wakulima wameonesha kuzikubali” anasema Dkt. Ligate 

Ingawa  wameanza na uzalishaji wa malisho,mtaalamu na mratibu  wa wa Teknolojia ya JUNCAO nchini Tanzania, Dkt Ligate ametoa wito kwa Watanzania kuwa tayari kuipokea na kuitekeleza tekinolojia hii kwa mapana yake ili kwamba Pamoja na uzalishaji wa malisho, lakini pia watazalisha Uyoga ili kujipatia kipato na kuhifadhi mazingira nchini Tanzania.

Wafugaji walioanza kuzalisha nyasi za Juncao, wamenufaika kwa kiasi kikubwa na wamekuwa na matokeo chanya ambapo wiki iliyopita Dkt Elly Ligate na Maafisa kutoka Wizara ya Mifugio na Uvuvi walitembelea mashamba yaliyoko Dodoma kujionea maendeleo ya nyasi za Juncao pia mashamba ya mfano kule visiwaniVisiwani Zanzibar na ili kuona jinsi hali inavyoendelea.

Dkt. Ligate ametoa shukrani kwa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Chuo Kikuu cha Fujiani cha Kilimo na Misitu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi Tanzania bara, Wizara ya Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo ya Zanzibar, pamoja na wadau binafsi kama vile Ndugu Albert Marwa kwa kufanikisha kuenea kwa tekinolojia ya Juncao nchini Tanzania.


 


Post a Comment

0 Comments