SUAMEDIA

Mkuu wa Wilaya ya Mbarali Mhe: Mfune apongeza SUA na WIOMSA kurejesha Afya na kupunguza madhara yanayotokana na uchafuzi wa Mazingira katika Mito

 

Na Amina Hezron,Mbeya

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia ufadhili wa Taasisi inayojishughulisha na tafiti za utunzaji wa Bahari (WIOMSA) wameendesha mafunzo ya Kimataifa ya kuwajengea uwezo Wanasayansi, Mameneja na wadau wengine namna ya kuendesha na kufanya tathimini ya Maji kwa Mazingira katika ukanda wa Magharibi mwa Bahari ya Hindi.


Mkuu wa Wilaya ya Mbarali Mkoani Mbeya Mhe. Mhe.  Reuben Mfune akifungua mafunzo hayo ya kimataifa ya kujengea uwezo wataalamu wa Tathimini ya Maji kwa  Mazingira, Pembeni yake ni Mkuu wa Mradi wa wa Utafiti wa  EFLOWS Prof. Japhet Kashaigili kutoka SUA.

Akifungua mafunzo hayo Septemba 19, 2022 Wilayani Mbarali Mkoani Mbeya, Mkuu wa Wilaya hiyo Mhe. Reuben Mfune amewataka wadau waliopata mafunzo hayo kuhakikisha wanakwenda kuyafanyia kazi na kuwafundisha wengine kwenye ofisi wanazotoka ili kutimiza malengo ya mafunzo.

 “Wale ambao wako ukanda wa juu ya mto unakoanzia wanatakiwa kujua fika shughuli za uharibifu wanazozifanya kule ndizo zinazoleta athari kwenye mabwawa ambayo yanajaa tope ambalo linakwenda mpaka Baharini na kuaathiri viumbe vilivyomo katika Mito, Maziwa na Bahari”, alisema Mhe. Mfune.

Mhe Mfune amewapongeza SUA na WIOMSA kwa kuandaa mafunzo hayo kwa kuwa yanaendana na kazi inayoendelea ya kurejesha afya ya Mito na kupunguza madhara yanayotokana na uchafuzi wa Mazingira katika mito, kwani ni jambo jema kufanyika na litakuwa msaada mkubwa kwa Taifa.

Aidha amewataka wadau wengine kuendelea kujitokeza kusadia jitihada za Serikali na wadau waliopo sasa ili kuhakikisha Mito inaendelea kutiririka mwaka mzima na hivyo kuwataka Wananchi kuheshimu Sheria zilizowekwa kwakuwa zipo kwa manufaa ya Watanzania wote.

Akizungumzia mafunzo hayo Mtafiti Mkuu wa Mradi huo kutoka SUA Prof. Japhet Kashaigili amesema lengo kubwa la mafunzo hayo ni kujenga Wataalamu na utaalamu wa kuweza kufanya tathimini ya maji kwa mazingira ili kusaidia wanapofanya maamuzi katika kugawana maji iwe kwa ajili ya maendeleo endelevu.

“Ni mafunzo ya kujenga uwezo ambayo yana vitendo ndani yake. Wataona shughuLi zinazofanyika kama sehemu ya kuhifadhi mazingira na kilichopelekea shughuLi hizo zifanyike pamoja na sababu za msingi za kuwezesha kwanini hiyo tathimini ya maji kwa mazingira ifanyike na shughuli gani zifanyike kwenye maeneo hayo. Hivyo mahari kwingine watafanya wao wenyewe kama sehemu ya mazoezi”, alisema Prof. Kashaigili.

Prof. Kashaigili amefafanua kuwa tathimini hiyo ya maji kwa mazingira itawezesha kuhusanisha madhara yanayotokana na shughuli mbalimbali zinazozifanywa na kwa kiasi gani zinapelekea kuathiri  Ukanda wote wa Bahari  ili kuweza kujua chanzo cha tatizo, hatua  tatizo lilipofikia, madhara na namna ya kutatua.

“Hii itasaidia nchi kutekeleza Sera ya Maji pamoja na Sheria ya maji ya mwaka 2009 ambayo imeainisha katika kugawana maji kwa vipaumbele ni kwa ajili ya matumizi ya Binadamu, Mazingira na kwa shughuli nyingine, hivyo maji kwaajili ya mazingira ilikuwa ni sehemu ambayo haina utaalamu na hakukuwa na jinsi ya kufanya hivyo bila kujenga utaalamu sasa utaalamu upo hivyo ni lazima tujenge sasa Wataalamu wengi “, alisema Prof. Kashaigili.

Kwa upande wake Meneja wa Programu ya Mazingira ya Bahari (WIOMSA) ambao ndio wafadhili wa mafunzo hayo, Dkt Mathias Igulu amesema kuwa kuna mahusiano makubwa kati ya Bahari na Mito, lakini jambo hilo halijaongelewa sana ndio maana WIOMSA wameona ni vyema kuanzisha mjadala na kuwaleta pamoja Wanasayansi na wadau wengine  kwa maslahi mapana ya uhifadhi wa Bahari, Mito na Mazingira.

“Kwa kushirikiana na Chuo chetu kikubwa cha SUA ambacho wote tunajua wana Wataalamu wabobevu kwenye maswala ya Sayansi za Kilimo, Maji na Mazingira, Ufugaji wa Samaki na Sayansi zingine zinazoendana na hizo tumeona ni muda muafaka kushirikiana nao kuwaleta pamoja wadau muhimu nchini na nje ya Tanzania kwa kuwa wanao uwezo mkubwa wa kusimamia”Alisema Dkt. Igulu.

Akizungumza mmoja ya washiriki wa mafunzo hayo, Mtafiti Msaidizi kutoka Taasisi ya Utafiti ya Uvuvi (TAFIRI) Bi. Wendo Lukwambe amesema mafunzo hayo yana umuhimu mkubwa kwao kwakuwa yatawasaidia kujua jinsi mtiririko wa maji unavyoenda na namna ya kutunza maji kwa mazingira kwakuwa isipofanyika hivyo itasababisha kuathirika kwa maji hayo.

Mafunzo hayo ya siku tano yamewahusisha washiriki kutoka Taasisi mbalimbali za Utafiti katika sekta za Maji, Mazingira, Misitu  na washiriki wengine kutoka nchi za ukanda wa magharibi mwa Bahari ya Hindi ikiwemo  Afrika Kusini, Kenya, Mauritius, Msumbiji, Visiwa vya Shelisheli, Somalia, , Visiwa vya  Comoro, Madagasca na Visiwa vya Reunion ambao wameshiriki kwa njia ya Mtandao (Zoom).


Mtafiti Mkuu wa Mradi huo kutoka (SUA) Prof. Japhet Kashaigili akieleza malengo ya Mafunzo hayo ya kujengea uwezo wataalamu wa masuala ya Maji kwa Mazingira na tathimini yake kutoka Nchi nzima nan chi zingine 11 za magharibi mwa bahari ya Hindi.







Meneja wa Programu ya Mazingira ya Bahari (WIOMSA) ambao ndio wafadhili wa mafunzo hayo, Dkt Mathias Igulu akitoa salamu za Taasisi yao umuhimu wa mafunzo hayo kwa nchi wanachama.

Post a Comment

0 Comments