SUAMEDIA

SUA kimeahidi kufanya kazi bega kwa bega na Wizara ya Afya ili kuibua Bunifu na kupata suluhisho la Kisayansi

 

Winfrida Nicolaus

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA kwa kushirikiana na Wizara ya Afya kimeahidi kufanya kazi bega kwa bega na wadau mbalimbali waliopo katika Mnyororo wa Thamani wa bidhaa za Tiba Asili kwaajili ya kuibua Bunifu na kupata suluhisho la Kisayansi kuhusu changamoto zilizopo kwenye Mnyororo wa Thamani wa Biashara ya Bidhaa za Mimea Dawa nchini.

Hayo yamebainishwa na  Mkurugenzi wa Uzamili, Utafiti na Uhaulishaji wa Teknolojia kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Prof. Esron Karimuribo Agosti 29, 2022 wakati akimwakilisha Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaalam Prof. Maulid Mwatawala ambaye alikuwa Mgeni Rasmi kwenye Kongamano la Kwanza la Kisayansi la Tiba Asili Tanzania linalofanyika SUA Kampasi Kuu ya Edward Moringe Sokoine.

Amesema uwepo wa Kongamano hilo la Kisayansi kuhusu Tiba Asili ya Mwafrika lililowakutanisha Wadau mbalimbali waliopo katika Mnyororo wa Thamani wa Bidhaa za Tiba Asili wakiwemo Wakulima wazalishaji, Wavunaji, Watengenezaji, Wauzaji wa jumla na rejareja , Taasisi zinazosimamia Ubora, Watunga Sera na Watafiti upo kwenye moja ya majukumu na malengo ya uanzishwaji wa SUA.

Prof. Karimuribo amesema wanaamini lengo la Kongamano hilo ni kuibua Bunifu na kupata suluhisho la Kisayansi kuhusu changamoto zilizopo kwenye mnyororo wa thamani wa biashara ya Bidhaa  za Mimea Dawa nchini ili bidhaa hiyo iwe endelevu na iweze kutoa mchango mkubwa kwenye kipato cha Wananchi kwa ujumla.

” Tunathamini sana mchango wa Sekta hii na tunaamini tukishirikiana kwa pamoja tutafika mbali hivyo nasisitiza katika suala la Ubunifu ili kuweza kuwa na Dawa Asili katika mfumo ambao unaweza kuupeleka kwenye Pharmacy ili tuweze kujua kilichopo ndani, dozi ni kiasi gani hata hivyo watafiti wameamua kujiongeza na kufanya Dawa hizi za Asili kuwa katika muundo wa kama dawa nyingine tunazotumia”, amesema Prof. Karimuribo

Aidha Prof. Karimuribo amewahakikishia wadau wa Kongamano hilo la Kwanza la Kisayansi la Tiba Asili Tanzania kuwa SUA kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania itakuwa bega kwa bega nao katika kuhakikisha kuwa yatokanayo na Kongamanola hilo yanapewa kipaumbele katika kazi zao za Utafiti, Mafunzo na kuwa endelevu ili kuboresha Bidhaa hizo za Tiba Asili.

Kwa upande wake Dkt. Paul Mhame kutoka Wizara ya Afya amekiomba Chuo cha SUA kuwasaidia kufanya Utafiti wa namna ya kulima na kupanda Miti Dawa katika kiwango kinachokubalika.

 

 

 










 

Post a Comment

0 Comments