SUAMEDIA

SUA kimeahidi kuendelea kushirikiana na Wizara ya Afya

 Editha Mloli

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA kimeahidi kuendelea kushirikiana na Wizara ya Afya katika mambo mbalimbali ambayo yanashabihiana na Mrengo wa Chuo katika kuisaidia jamii hasa wale wanaohusika na masuala ya Tiba Asili na Tiba Mbadala na kufanyia kazi mapendekezo yaliyotolewa katika Kongamano la Kwanza la Tiba Asili ya Mwafrika hapa nchini.

Hayo yamezungumzwa na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine Cha Kilimo SUA Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaalam Prof. Maulid Mwatawala wakati akifunga Kongamano la Kwanza la Tiba Asili ya Mwafrika lililofanyika Mjini Morogoro katika Chuo cha SUA.

Prof. Mwatawala amesema Chuo kitazibeba changamoto pamoja na mapendekezo yaliyotolewa na Wadau wa Tiba Asili na Tiba Mbadala  na kuona namna gani  kitakavyoyafanyia kazi ili koberesha sekta hiyo .

Aidha Prof. Mwatawala amewataka Wadau wa Tiba Asili na Tiba Mbadala kuendelea kushirikiana na Chuo cha SUA na kutumia fursa mbalimbali zinazopatikana ili kusaidia kutengeneza bidhaa zenye ubora, upatikanaji wa masoko na mazingira bora. 

Mhadhiri Mwandamizi kutoka SUA Dkt. Gay Merry Bakari ambaye ni kati ya Watafiti ambao wameweza kuwasilisha kuhusiana na Tafiti ya Mmea alioufanyia kazi na ambao umeleta matokeo chanya amesema alianza kufanyia majaribio kwenye jeraha la Panya ili kuona kama dawa hiyo inaweza kuponya vidonda na ikafanikiwa ambapo mpaka sasa zaidi ya watu 18 wamepona vidonda kutokaa na dawa hiyo aliyoitengeneza kutokana na mmea dawa.

Akiwasilisha moja ya mmea unaofahamika kwa jina la Mvunjakongo Mwanafunzi wa Shahada ya Uzamili na Mtafiti kutoka SUA David Credo amesema majani ya mti huo hutumika kutengeneza dawa ya kudhibiti na kutibu kideri kwa kuku, kudhibiti virusi katika mayai ya kuku, na kuongeza kuwa kemikali yake ikitumika viwandani itasaidia kuzalisha dawa kwa ajili ya kuku.

Kongamano hilo la siku mbili ambalo lilianza Agosti 29 na kuhitimishwa Agosti 30, 2022 limeambatana na Mdahalo kuhusiana na Usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa ambao umehusisha Wadau mbalimbali wanaohusika na Tiba Asili wakiwemo SUA, Wizara ya Afya, TIRDO, GCLA, pamoja na Waganga wa Tiba Asili kutoka mikoa yote Tanzania.

Maadhimisho ya 20 ya Wiki ya Tiba Asili ya Mwafrika yameadhimishwa kitaifa mkoani Morogoro ambayo yanatarajiwa kuhitimishwa Agosti 31, yakiwa na kauli mbiu “Miongo miwili ya Tiba Asili ya Mwafrika kuelekea huduma za Afya kwa wote”.




Post a Comment

0 Comments