Amina Hezron
Serikali imeshauriwa kufanya mapitio ya kuona namna bora ya
kuboresha viwango vya bidhaa zitokanazo na rasilimali misitu hususani mkaa
unaozalishwa kwa njia endelevu kutokana na bidhaa hiyo kutumiwa na watu wengi
nchini.
Ushauri huo umetolewa Agost 26 mkoani Morogoro katika Warsha
ya Uthibitishaji wa Mazao ya Misitu
Tanzania iliyoandaliwa na Shirika la Kuhifadhi Misitu ya Asili nchini Tanzania
(TFCG) na Mtaalamu wa Uthibitishaji wa Misitu na Mazao ya Misitu kutoka Kampuni
ya EFC Dkt. Severine Kalonga
Dkt. Severine Kalonga amesema takwimu zinaonesha asilimia 70
ya watanzania wanatumia nishati inayotokana na rasilimali misitu na hitaji la
mkaa uliothibitishwa nchini bado ni mdogo kutokana na uwepo wa uzalishaji
holela unaofanyika hivyo amewataka wauzaji kutambua thamani ya kuwa na mkaa
uliothibitishwa ikiwemo uwepo wa ongezeko la gharama za uuzaji kutokana
ongezeko la ubora .
“Nishati itokanayo na kuni ama mkaa ni nishati inayohitajika
na kutumika na watanzania wengi hivyo bila kuweka viwango vya uthibiti wa namna
ya kuzalisha mkaa kwa njia endelevu tutaendelea kupata changamoto ya uharibifu
wa mazingira na misitu nchini”, alisema Dkt. Kalonga.
Kwa upande wake Bw.
Yuvenal Pantaleo ambaye ni Meneja Uthibitishaji kutoka Shirika la Mpingo
Conservation and Development Initiative
(MCDI) amesema kwa upande wao tangu wamefanikiwa kupata uthibitishaji wa mbao
kumekuwa na mabadiliko makubwa ya bei za mbao pamoja na kupata soko la uhakika
la nje ya nchi kauli ambayo inaungwa mkono na Isaya Saitabau ambaye ni Meneja
wa Msitu wa Jamii wa SULEDO.
Aidha Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii inaandaa
Muongozo na Mkakati wa Taifa wa Matumizi endelevu ya Mazao ya Mkaa ili
kuhakikisha mkaa unapovunwa na kutumiwa ni kwa maendeleo endelevu jambo
litakalofanyika kwa kuzingatia mnyororo wa thamani kuanzia uvunaji mpaka hatua
ya masoko.
Akieleza hayo
Mwakilishi wa Wizara ya Maliasili na Utalii James Nshare amesema licha
ya kuwepo kwa matumizi ya nishati zingine mbadala za gesi na umeme lakini bado
watanzania walio wengi wanafanya matumizi ya nishati ya mkaa hivyo kutaka
uvunwe na kutumiwa kwa njia endelevu
bila kuathiri misitu.
“ Kuna changamoto iliyopo ni vigumu sana kutofautisha mkaa
uliovunwa kihalali na ambao haujavunwa kihalali
katika masoko hilo bado ni tatizo katika eneo la uthibiti lakini bado
kupitia mkakati huu unaoandaliwa kuna mbinu ambazo zimeainishwa kama zitakwenda
kusimamiwa zitasaidia kutatua changamoto hiyo”, alisema Nshare.
Aidha Nshare amefafanua kuwa suala la mkaa bado ni changamoto
na linahitaji ushiriki wa wadau na sekta mbalimbali katika kuhakikisha
unatumiwa kwa njia sahihi .
Warsha hiyo hiyo ya siku mbili ya Uthibitishaji wa Mazao ya
Misitu iliyoandaliwa na TFCG kupitia mradi wa CoFoReST unaofadhiliwa na Shirika
la Maendeleo na Ushirikiano la Uswizi(SDC) imeshirikisha wadau mbalimbali kama
vile Shirika la Kuhifadhi Mpingo na Maendeleo (MCDI) TAFORI,SUA,TAMISEMI na
Wizara ya Maliasili na Utalii.
0 Comments