SUAMEDIA

SUA kuwajengea uwezo wanafunzi jinsi ya kupambana, kudhibiti magonjwa sugu yasiyoambukiza pamoja na Ukimwi

 

Winfrida Nicolaus

Kutokana na tafiti mbalimbali duniani zinazoonesha kwamba watu wa rika mbalimbali hujifunza na kuzingatia zaidi mafunzo iwapo yatatolewa na watu wenye umri, jinsia na shughuli zinazofanana, Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeendelea kuwajengea uwezo wanafunzi toka kwenye kozi mbalimbali chuoni hapo ili waweze kusaidia kutoa elimu ya jinsi ya kupambana na kudhibiti magonjwa sugu yasiyoambukiza (MSY) pamoja na Ukimwi.

Hayo yameelezwa na Kaimu Mkurugenzi, Kurugenzi ya Shahada za Awali katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Dkt. Alex Matofali wakati akifungua mafunzo kuhusiana na namna bora za kudhibiti na kupambana na magonjwa sugu yasiyaambukiza (MSY) Pamoja na Ukimwi kwa baadhi ya wanafunzi chuoni hapo ambao wataenda kuwa mstari wa mbele katika kuelimisha jamii pamoja na wenzao.

Dkt. Matofali amesema kuwa magonjwa sugu yasiyoambukiza Pamoja na Ukimwi yamekuwa yakiuchangia ulemavu (disability) na vifo vingi kwa vijana na watu wa rika mbalimbali na madhara hayo yameongezeka sana katika miaka ya karibuni ambapo kwa mwaka 2016/2017 imebainika kwamba sehemu kubwa ya maambukizi mapya ya VVU yanatokea kwa vijana wenye umri kati ya miaka 15 – 23 kundi ambalo wengu wao kwa sasa wapo vyuoni.

Aidha amesema hivi sasa familia na serikali zimekuwa zikiwekeza sana katika suala la elimu ya juu, lengo na madhumuni ya uwekezaji huo ni kuhakikisha wanafunzi wanapata ujuzi ili waweze kusaidia familia zao na kuchangia katika maendeleo ya taifa kwa ujumla hata hivyo pamoja na dhamira zao nzuri iko hatari kwa ndoto hiyo kufutika kutokana na athari za VVU/UKIMWI na Magonjwa sugu yasiyoambukiza (MSY).

Unajua acha tu niseme magonjwa sugu yasiyoambukiza kwa sasa yamekuwa ni hatari sawa na Ukimwi na yamekuwa yakisababisha vifo vingi pamoja na ulemavu na kwa bahati mbaya zaidi magonjwa sugu yasiyoambukiza yamekuwa yakisababishwa kwa sehemu kubwa na mienedo ya maisha kuanzia umri mdogo. Ni kwa msingi huo imelazimu kuanza kutoa elimu kuhusu magonjwa tajwa kwa lengo la kuchukua hatua madhubuti mapema”. Amesema Dkt. Alex Matofali.

Kwa upande wake Dakatari bingwa wa magonjwa ya wanawake kutoka katika Hospitali ya SUA Dkt. Elimwidim Swai amesema kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) watu zaidi ya Millioni Moja wanaathirika na magonjwa yanayoambukizwa kwa njia ya Ngono (STI) kila mwaka na hivyo wameamua kutoa elimu kila wakati kwa jumuiya ya SUA ili kupunguza maambukizi kwa kizazi hiki na kijacho.

Ameyataja madhara yatokanayo na magonjwa yanayoambukizwa kwa njia ya ngono kuwa ni pamoja na kushindwa kuzaa, mimba kutunga nje ya kizazi kwa wanawake, kupata saratani, wanawake kujifungua kabla ya wakati (premature), au kujifungua mtoto aliyefariki.

Ili kujilinda sisi pamoja na wenza wetu katika magonjwa haya yanayoambukiza kwa njia ya ngono hususani ukimwi tunapaswa kuwa  waaminifu kwa wenza wetu yani tusiwe na mpenzi zaidi ya mmoja lakini pale inapobainika mmoja wetu ameathirika na ugonjwa huu tujitahidi kufuata masharti ya wataalamu wa afya na kutumia kinga kwa usahihi lakini pia tujiepushe kushirikiana vitu vyenye ncha kali kama nyembeAmesema Dkt. Swai.

 




Post a Comment

0 Comments